Mnadhimu wa Jeshi la Sudan Yasser al-Atta amesema jeshi lilikuwa linashambulia kutoka pande zote kwa lengo la kuwaangamiza wapiganaji wa Rapid Support Forces (RSF) kabla ya mwisho wa mwaka.
Al-Atta alizungumza siku ya Jumatatu kabla ya wapiganaji kukusanyika kulingana na video zilosambazwa na wanaounga mkono jeshi kwenye mitandao ya kijamii, Sudan Tribune iliripoti.
Eneo walilokusanyika halijabainika.
“"Tunatekeleza mpango wa kuvamia kutoka pande zote, huku sote tukishambulia kwa wakati mmoja, kama ilivyofanyika wakati wa kudhibiti tena Khartoum," amesema al-Atta.
“Kabla ya mwisho wa mwaka huu, hakutakuwa na mpiganaji hata mmoja wa Janjaweed,” alisema, akitumia jina hilo kumaanisha RSF, “au mpiganaji wa kigeni, na tuna nia ya kutimiza hilo.”
Mafanikio ya jeshi
Maelezo ya Al-Atta yanakuja siku kadhaa baada ya jeshi na vikosi washirika kufanya operesheni ya kufanikisha kudhibiti maeneo ya Bara, Jabra al-Sheikh, Um Sayala na maeneo mengine pamoja na barabara inayounganisha Omdurman na El-Obeid Kaskazini mwa Kordofan.
Kumekuwa na mapigano makali kati ya jeshi na RSF kuanzia Oktoba 2025 katika majimbo matatu ya Kordofan - Kaskazini, Magharibi na Kusini.
Mapigano kati ya jeshi la Sudan na RSF, yalianza Aprili 2023, na yamesababisha vifo vya maelfu ya watu na kulazimisha watu karibu milioni 13 kuondoka katika makazi yao, kulingana na Umoja wa Mataifa na tathmini ya kimataifa.




















