Uturuki haitokaa kimya wakati Israel inalitumbikiza eneo zima katika umwagaji damu: Erdogan

Erdogan alisisitiza kuwa Uturuki haitabagua mataifa jirani wala kunyamaza mbele ya mateso ya watu wa eneo hilo.

By
Rais alishutumu uongozi wa Israel kwa kupanua malengo yake ya kimkakati katika eneo hilo. / / AA

Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, ameonya kuwa vita vilivyoanzishwa dhidi ya Iran vinaisukuma Mashariki ya Kati zaidi kwenye hali ya kutokuwa na utulivu, akimtuhumu Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, kwa kupanua mgogoro katika eneo hilo.

Akizungumza katika mkutano wa viongozi wa majimbo wa chama cha Haki na Maendeleo (AK Party) katika kituo cha mikutano cha chama hicho jiini Ankara siku ya Alhamisi, Erdogan alisema vita hivyo vimeingiza eneo hilo katika mojawapo ya vipindi vyenye maumivu makali zaidi ya karne iliyopita.

“Vita vilivyoanza dhidi ya Iran vinaendelea kulizamisha eneo letu katika harufu ya damu na baruti,” alisema Erdogan.

“Watoto wasio na hatia wanakuwa walengwa wa makombora wakiwa wameketi madarasani mwao.”

Rais huyo wa Uturuki alieleza hali ya sasa kama hatua muhimu ya kihistoria kwa Mashariki ya Kati, akionya kuwa chuki na msimamo mkali wa kiitikadi wa Israel vinausukuma ukanda huo kuelekea maafa.

“Eneo letu linaishi katika siku zenye maumivu makali zaidi ya karne iliyopita,” alisema.

“Mtandao wa mauaji ya kimbari uliopofushwa na chuki unavuta jiografia yetu kuelekea janga huku ukijificha nyuma ya hoja za kidini.”

Erdogan alisisitiza kuwa Uturuki haitabagua kati ya mataifa jirani wala kunyamaza wakati watu wa eneo hilo wakiteswa.

“Kila mtu ajue hili: hatubagui kati ya ndugu na majirani zetu, na hatutawahi kupuuza maumivu yao,” alisema.

“Kama Uturuki na taifa la Kituruki, hatuwaachi watu tunaowaona kama marafiki na ndugu katika nyakati ngumu.”

Lebanon

Kwa mujibu wa Erdogan, serikali ya Netanyahu hailengi Iran pekee bali pia inaendelea hatua kwa hatua kutekeleza mipango ya kuikalia Lebanon.

Kwa karibu mwezi mmoja, Erdogan alisema mashambulizi yanayoendelea yamepuuza kanuni na misingi yote ya kimataifa.

Alihoji kama wanaotekeleza mashambulizi hayo wanaona tofauti yoyote kati ya utambulisho wa watu wanaoathiriwa na vurugu hizo.

“Kwa siku 27, washambuliaji wanaopuuzia kila kanuni, thamani na desturi wametuonyesha jambo la wazi,” alisema.

“Kwa macho yao, kuna tofauti gani ikiwa sisi ni Washia au Wasunni, Waturuki, Wakurdi, Waarabu au Waajemi?”

Akionyesha huzuni kubwa kuhusu idadi ya vifo vya raia, Erdogan alielekeza macho kwenye huzuni ya pamoja inayohisiwa katika eneo hilo.

“Kwa moyo unaovuja damu, nauliza: kuna tofauti gani kati ya machozi yanayomwagika Isfahan na Tehran na yale yanayomwagika Erbil, Baghdad, Beirut au Riyadh?”

Ingawa alielezea mgogoro huo kama kimsingi ni vita vya Israel, Erdogan alisema athari zake zinahisiwa na watu wengi zaidi.

“Hivi vinaweza kuwa vita vya Israel, lakini gharama kubwa inalipwa kwanza na Waislamu na hatimaye na binadamu wote,” alisema.

Mikakati ya Kizayuni

Erdogan pia alionya dhidi ya juhudi za kuongeza mgawanyiko miongoni mwa jamii za eneo hilo, akizishutumu mikakati ya Kizayuni kwa kujaribu kuchochea mivutano ya kidini na kikabila.

“Tunakataa hatua au mijadala yoyote itakayochochea uhasama miongoni mwa watu wa kindugu au kuunga mkono mipango ya ‘kugawa watu kwa misingi ya kuwautawala’ ya Uzayuni inayolenga eneo letu,” alisema.

Rais huyo wa Uturuki alisema kwamba baada ya sauti za mabomu na makombora kupotea, watu wa Mashariki ya Kati bado watalazimika kuishi pamoja.

“Baada ya sauti za mabomu na makombora kunyamaza, tutaendelea kuishi pamoja katika eneo hili,” alisema Erdogan. “Hakuna anayepaswa kusahau ukweli huu.”

Erdogan pia alilaani vizuizi vya ibada kwa Waislamu katika Msikiti wa Al-Aqsa, akisema kuwa kwa mara ya kwanza tangu 1967, swala ya Idi haikufanyika katika eneo hilo takatifu.

“Ukosefu huu wa sheria ni shambulio la kiburi dhidi ya imani ya Waislamu bilioni mbili,” alisema, akiongeza kuwa haki ya Waislamu kuabudu katika Al-Aqsa haiwezi kuzuiwa kwa hali yoyote.

Akithibitisha tena msimamo wa kidiplomasia wa Uturuki, Erdogan alisema Uturuki itaendelea kufuata sera ya nje inayozingatia amani na utulivu.

“Hatutarudi nyuma kutoka kwenye sera yetu ya nje ya amani inayojengwa juu ya kanuni ya amani kwa wote, utulivu kwa wote na ustawi kwa wote,” alisema.