Uturuki imekuwa na nafasi muhimu katika kuanzisha na kuendeleza mazungumzo kati ya Serikali ya Somalia na makundi ya upinzani, wakati nchi hiyo ikikabiliwa na mjadala kuhusu marekebisho ya Katiba na mfumo wa uchaguzi, kwa mujibu wa vyanzo vya usalama vilivyozungumza na shirika la habari la Anadolu Agency.
Mazungumzo hayo yalianza Jumanne jijini Mogadishu kufuatia juhudi za Shirika la Ujasusi la Uturuki (MIT), baada ya kuzuka kwa tofauti za maoni kuhusu mabadiliko yaliyopendekezwa katika Katiba na mfumo wa uchaguzi.
Vyanzo hivyo vinasema juhudi za muda mrefu za MIT, zilizotekelezwa kwa maelekezo ya Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, zimezaa matokeo chanya. Wawakilishi wa Serikali ya Somalia na viongozi wa upinzani wamekubaliana kuendeleza mazungumzo hayo, huku mchakato huo ukifanyika kwa uratibu wa karibu na Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki.
Kujenga imani
Vyanzo hivyo vinaeleza kuwa MIT imekuwa ikifanya kazi kwa muda mrefu ya kujenga imani kati ya wadau wa kisiasa nchini Somalia na kusaidia kutatua migogoro kupitia mazungumzo yenye msingi wa kujenga.
Katika kipindi chote cha mchakato huo, Uturuki imeendelea kusisitiza kuwa amani ya kudumu na utulivu nchini Somalia vinaweza kupatikana kupitia mazungumzo, maridhiano na mchakato wa kisiasa unaowashirikisha wote. Aidha, imeweka bayana kuwa mustakabali wa Somalia unapaswa kuamuliwa na Wasomali wenyewe.
Vyanzo vya usalama viliongeza kuwa Uturuki, kama rafiki wa dhati na mshirika wa kimkakati wa Somalia, itaendelea kuchangia juhudi za kuimarisha amani, utulivu na maendeleo nchini humo.
Kwa upande wake, Serikali ya Somalia iliishukuru Uturuki kwa nafasi yake ya upatanishi, ikisema kuwa mkutano kati ya wawakilishi wa serikali na upinzani ulifanyika jijini Mogadishu katika mazingira ya kirafiki.
"Tulipata fursa ya kubadilishana mawazo kwa uwazi, kwa dhati na kwa njia yenye kujenga," ilisema serikali katika taarifa yake, huku pande zote zikitoa shukrani kwa Uturuki kwa jukumu lake la kuwezesha mazungumzo hayo.
Rais wa zamani wa Somalia, Mohamed Abdullahi Farmaajo, ambaye alihudhuria mazungumzo hayo kwa niaba ya sehemu ya upinzani, alisema pande zote zimekubaliana kuendelea na mchakato wa mazungumzo jumuishi kwa lengo la kuimarisha utulivu wa kisiasa, usalama na ustawi wa Somalia.












