Simu ya mkononi iliyonyanyuliwa mbele ya kamera ya televisheni ikawa moja ya picha mashuhuri zaidi za jaribio la mapinduzi lililoshindwa nchini Uturuki tarehe 15 Julai 2016, wakati kundi la wanajeshi waasi waliokuwa watiifu wa Shirika la Kigaidi la Fetullah (FETO) walipojaribu kuipindua serikali iliyochaguliwa kidemokrasia.
Rais Recep Tayyip Erdogan, akiwa anaonekana kupitia mtandao wa FaceTime kwenye kituo cha habari cha CNN Türk, aliwahimiza wananchi watoke mitaani na kupinga jaribio hilo la mapinduzi ya kijeshi.
Haikuwa hotuba iliyotolewa jukwaani wala taarifa rasmi iliyotolewa kupitia taratibu za kawaida za dola. Ilikuwa ya dharura, ya karibu na ya kisasa kabisa: mkuu wa nchi akilihutubia taifa kupitia kifaa kilekile ambacho wananchi walikitumia kuwasiliana na familia zao, kufuatilia habari za papo kwa papo na kuelewa kilichokuwa kinaendelea katika usiku wa hofu.
Umuhimu wa tukio hilo haukuwa wa kiteknolojia pekee. Ulikuwa wa kisiasa, kitamaduni na kijamii. Wakati waasi walipojaribu kuonyesha kwamba kila kitu tayari kilikuwa kimeamuliwa, mahojiano hayo ya FaceTime yalivunja taswira hiyo.
Yalidhihirisha kwamba uongozi uliochaguliwa ulikuwa bado unazungumza, wananchi walikuwa bado wanapewa maelekezo, na kwamba hatima ya usiku huo ilikuwa bado haijaamuliwa.
Mwonekano huo ulikuwa muhimu. Mapinduzi hayategemei nguvu pekee, bali pia mtazamo wa watu. Wapangaji wa mapinduzi hujaribu kuwashawishi wananchi, taasisi na vyombo vya usalama kwamba ukaidi hauna maana, kwamba mamlaka tayari yamehamia upande mwingine, na kwamba njia salama ni kukaa kimya.
Kuonekana kwa Rais Erdogan kulibadilisha mtazamo huo papo hapo. Ingawa picha hiyo ilikuwa rahisi, athari yake ilikuwa kubwa: skrini ndogo ikawa ishara ya kitaifa kwamba siasa za kawaida hazikuwa zimesalimu amri mbele ya nguvu za mabavu.
Jaribio la mapinduzi lilifuata mantiki ya zamani ya matumizi ya nguvu. Vifaru viliingia madarajani, wanajeshi wakajaribu kuteka viwanja vya ndege, barabara na vituo vya televisheni.
Waasi walielewa, kama wapangaji wengi wa mapinduzi katika historia, kwamba kudhibiti alama zinazoonekana za mamlaka ni jambo muhimu. Katika karne ya ishirini, kuteka kituo cha utangazaji kulitosha kuwafanya watu waamini kwamba dola tayari ilikuwa imebadilisha uongozi.
Lakini mwaka 2016, Uturuki haikuwa tena ikiishi katika mazingira hayo ya mawasiliano. Uwanja wa mijadala ya umma haukutegemea studio moja, mtambo mmoja wa utangazaji au tangazo moja rasmi.
Uliishi kupitia mamilioni ya simu za mkononi, kurasa za mitandao ya kijamii, ujumbe, matangazo ya moja kwa moja na makundi ya familia. Hivyo basi, jaribio la mapinduzi halikukutana tu na upinzani wa kisiasa, bali pia na utamaduni mpya wa ushiriki wa kiraia.
Ndiyo maana simu kupitia mtandao wa FaceTime haipaswi kutazamwa kama tukio la kusisimua la vyombo vya habari pekee. Ilikuwa daraja kati ya utangazaji wa kawaida na hatua za kiraia zilizounganishwa kwa njia ya kidijitali.
Vyombo vya habari vya kimataifa vilifanya ujumbe huo uonekane kitaifa, lakini mara moja ulienea kupitia mitandao ya kijamii, programu za mawasiliano, simu za kawaida na mawasiliano ya ana kwa ana. Kilichoanza kama picha kwenye televisheni kiligeuka kuwa kichocheo cha hatua za wananchi.
Kutoka mitandao ya kidijitali hadi hatua za kiraia
Nadharia za harakati za kijamii hutusaidia kuepuka tafsiri rahisi ya usiku huo. Mitandao ya kijamii haikusababisha uhamasishaji. Badala yake, iliharakisha mambo matatu muhimu kwa hatua za pamoja wakati wa mgogoro: uelewa wa pamoja wa kinachoendelea, njia zinazoonekana za kuhamasisha watu, na imani kwamba wengine pia walikuwa wakichukua hatua.
Mwanasosholojia na mwanasiasa wa Marekani Charles Tilly alisisitiza umuhimu wa kuelewa jinsi mbinu ambazo watu hutumia kudai haki zao zinavyobadilika.
Mnamo Julai 15, miaka kumi iliyopita, mbinu za wananchi wa Uturuki hazikujumuisha tu kukusanyika viwanjani na kusimama mbele ya vifaru, bali pia kurusha matangazo ya moja kwa moja, kushiriki maeneo walikokuwa, kusambaza wito wa kupinga mapinduzi, kurekodi matukio na kutumia vifaa vyao binafsi kuratibu juhudi za umma.
Kufuatia hatua hizo watu walizidi kujitokeza.
Hili halikuwa suala la majukwaa ya kidijitali pekee. Tafiti za Profesa wa Sosholojia Alev Erkilet wa Chuo Kikuu cha Ibn Haldun zinaonyesha kwamba tabaka la kidijitali haliwezi kueleweka bila kuzingatia maadili ya jamii, mitandao ya kiraia na hisia ya kuwa sehemu ya umma nchini Uturuki.
Twitter, Facebook, Periscope na programu za mawasiliano zilikuwa muhimu kwa sababu ziliunganishwa na mahusiano yaliyokuwepo tayari ya kuaminiana, uwajibikaji na utambulisho wa pamoja.
Majirani walitahadharishana kuhusu hatari. Misikiti ilitoa matangazo. Vituo vya televisheni viliendelea kurusha matangazo. Viongozi wa kisiasa na wananchi wa kawaida walieneza wito wa kupinga mapinduzi.
Mitandao ya kidijitali na mitandao ya kijamii ilifanya kazi kwa pamoja.
Mwanasheria na mwanafalsafa wa siasa wa Ujerumani Carl Schmitt aliwahi kusema kwamba mamlaka ya dola yanahusiana na uwezo wa kuamua wakati wa hali ya dharura.
Kwa maana fulani, mapinduzi ni jaribio la kutwaa hali hiyo ya dharura ili kusimamisha siasa za kawaida na kulazimisha uhalisia mpya kwa nguvu.
Mnamo Julai 15, mwitikio wa wananchi ulikataa kuruhusu nguvu za mabavu ziwe pekee zinazounda uhalisia wa kisiasa. Wananchi hawakupokea taarifa tu; walizitafsiri, walizifanyia kazi na walisaidia kuamua maana ya mgogoro huo.
Mapambano hayo yalikuwa muhimu sana. Usiku huo ungeweza kutazamwa kama tatizo la usalama ambapo wananchi wangetakiwa kubaki majumbani wakisubiri.
Badala yake, ulieleweka kama shambulio dhidi ya demokrasia yenyewe, ambalo wananchi walikuwa na wajibu wa kulipinga.
Kuonekana kwa Rais Erdoğan kupitia mtandao wa FaceTime kulikuwa tukio muhimu lililoelekeza uelewa huo.
Kulitoa ujumbe wazi kwa wananchi waliokuwa wametawanyika wakati wa sintofahamu: mgogoro huo ulihitaji hatua za kiraia, si kutazama kimya kimya.
Video ya mtu mmoja ikawa uthibitisho kwa mwingine. Wito mmoja wa kukusanyika ukawa mlolongo wa uhamasishaji.
Picha moja ya ukaidi ikaenea kwa kasi kuliko juhudi za kuzima sauti za wananchi.
Kwa hiyo, umuhimu wa FaceTime haukuwa tu kwamba ulimwezesha Rais Erdogan kuzungumza.
Ulikuwa ni ujumbe ambao uliingia katika mfumo mpana wa mawasiliano ambapo wananchi waliweza kuusikia, kuurudia, kuuthibitisha, kuusambaza na kuchukua hatua.
Bila shaka, kasi hiyo hiyo ya mawasiliano ilisababisha pia mkanganyiko.
Uvumi ulienea. Taarifa zinazokinzana zilisambaa. Video halisi zilichanganyika na madai ambayo hayakuwa yamethibitishwa.
Tafakari ya kweli kuhusu Julai 15 lazima ikubali ukweli huu wa pande mbili: majukwaa ya kidijitali yanaweza kuzalisha nguvu kubwa ya kiraia na wakati huohuo kusababisha vurugu za taarifa.
Hata hivyo, ukweli muhimu unabaki kwamba uhamasishaji wa mtandaoni uliwarudisha wananchi mitaani.
Hatua muhimu zaidi haikuwa kuchapisha ujumbe, bali kujitokeza: kwenye madaraja, viwanjani, nje ya viwanja vya ndege, mbele ya majengo ya serikali za mitaa na vituo vya habari.
Mitandao ya kijamii haikuchukua nafasi ya ujasiri. Iliufanya ujasiri huo uonekane, uenee na uratibiwe.
Kuundwa wa kumbukumbu ya kidijitali ya kiraia
Muongo mmoja baadaye, Julai 15 imekuwa sehemu ya kumbukumbu ya pamoja ya kidijitali ya Uturuki.
Kila mwaka kumbukumbu hiyo huibuka tena kupitia video za zamani, matangazo ya moja kwa moja, picha za skrini, ushuhuda na heshtegi.
Picha ya FaceTime hujitokeza kwa nguvu zaidi kwa sababu inabeba maana ya usiku mzima kwa namna iliyorahisishwa: wakati ambapo mamlaka ya kisiasa, mawasiliano ya umma na ushiriki wa wananchi vilipitia kwenye mitandao ya kijamii kabla ya kurejea mitaani.
Sehemu ya kumbukumbu hiyo huandaliwa rasmi na serikali, lakini sehemu kubwa hubebwa na wananchi wa kawaida wanaoshiriki tena walichokiona, walipokuwa, waliowapoteza na wanachokikumbuka.
Hivyo ndivyo kumbukumbu ya pamoja inavyofanya kazi ambayo zamani ilitekelezwa zaidi na makaburi ya kumbukumbu, sherehe rasmi na vitabu vya shule.
Leo, kumbukumbu ya Julai 15 haiishi tu katika viwanja vya umma na hotuba rasmi, bali pia katika video zilizohifadhiwa, mazungumzo ya familia, machapisho ya zamani ya Twitter na picha zinazorejea kila mwaka kwenye mitandao ya kijamii.
Kwa watu wengi, kumbukumbu ya usiku huo haiwezi kutenganishwa na vifaa walivyovitumia kuushuhudia: tahadhari ya kwanza, video ya kwanza, simu ya kwanza kutoka kwa ndugu na matangazo ya kwanza ya moja kwa moja yaliyowafanya watambue ukubwa wa hatari.
Huenda maisha hayo ya kitamaduni baada ya tukio yakawa mojawapo ya urithi wa kudumu zaidi wa Julai 15.
Majukwaa ya kidijitali huibuka, hupungua, hubadilishwa majina au hutoweka.
Lakini mienendo ya kiraia iliyoonekana usiku huo imeendelea kuwepo: wakati taifa linapokabiliwa na mgogoro, wananchi hutumia njia zozote zilizopo kuhamasisha, kurekodi, kutafsiri na kuhifadhi kumbukumbu.
Hapa ndipo Julai 15 pia inapochangia mjadala wa sasa kuhusu mamlaka ya kidijitali.
Mara nyingi dhana hiyo huzungumziwa kwa mtazamo wa kiufundi au wa kijiografia wa kisiasa: miundombinu, data, kanuni, majukwaa na uwezo wa taifa. Masuala hayo ni muhimu.
Lakini Julai 15 inaonyesha upande mwingine pia. Mamlaka ya kidijitali pia yanahusu uwezo wa jamii kuhifadhi sauti yake ya umma wakati nguvu za mabavu zinapojaribu kutawala kabisa sehemu ya mawasiliano ya umma.
Jibu la usiku huo halikutokana na teknolojia pekee. Lilitokana na mwingiliano kati ya zana na watu, mitandao ya kijamii na mitaa, pamoja na uongozi wa kisiasa na ushiriki wa wananchi.
Uturuki haikuingia mtandaoni tu mnamo Julai 15. Iliutumia ulimwengu wa kidijitali kama njia ya kurejea katika maisha ya umma.
Ndiyo maana kumbukumbu ya kidijitali ya Julai 15 inaendelea kuwa na nguvu kubwa.
Haikumbukwi tu kama usiku wa mizinga na ndege za kivita, bali pia kama usiku wa simu zilizoinuliwa sebuleni, video zilizowekwa kwa hofu, ujumbe uliotumwa kwa wapendwa, na wananchi waliogundua kwa wakati halisi kwamba hawakuwa peke yao.
Jaribio la mapinduzi lililenga kudhoofisha matakwa ya kidemokrasia kwa kudhibiti maeneo, kueneza hofu na kuhodhi mawasiliano.
Lakini mwitikio wa wananchi ulionyesha kwamba katika enzi ya kidijitali, maisha ya kiraia ni magumu zaidi kunyamazishwa kuliko ilivyokuwa hapo awali.
Watu walizidi kumiminika viwanjani. Si mitaani pekee, bali pia katika kila mkono ulioshika simu, kila ujumbe uliowatia watu moyo, na kila mwananchi aliyebadilisha taarifa kuwa hatua.



















