Viongozi wa dunia wanakusanyika Uturuki katika Mkutano wa 5 wa Diplomasia wa Antalya

Zaidi ya viongozi 20 wa nchi na mawaziri 50 wa mambo ya kigeni watashiriki katika Mkutano wa Diplomasia wa Antalya 2026 ili kujadili changamoto za kisiasa, kiuchumi na kikanda.

By
Jukwaa la Diplomasia la Antalya 2026 litakuwa na zaidi ya vikao 40 vinavyozungumzia changamoto za kisiasa na kiuchumi duniani. Picha/Maktaba

Mji wa utalii wa Antalya, Uturuki, utakuwa tena kitovu cha diplomasia ya kimataifa Aprili hii, wakati viongozi wa dunia, mawaziri na maafisa wakuu watakavyokusanyika katika moja ya majukwaa mashuhuri kimataifa kwenye kalenda.

Ikiwa chini ya kaulimbiu 'Kupanga Kesho, Kusimamia Kutokuwa na Uhakika', Jukwaa la Diplomasia la Antalya 2026 (ADF2026) litaleta pamoja viongozi kujadili kutokuwepo kwa utulivu duniani na kuunda mustakabali wa diplomasia ya kimataifa.

Jukwaa la tano la Diplomasia la Antalya litafanyika Antalya kuanzia Aprili 17 hadi 19.

Tangu kuanzishwa kwake mwaka 2021, jukwaa limekua taratibu hadi kuwa jukwaa kinara katika mazungumzo, ushirikiano, na ushiriki wa ngazi ya juu wa diplomasia duniani kote.

Toleo la mwaka huu linatarajiwa kuwa mwenyeji wa wawakilishi kutoka nchi zaidi ya 150, wakiwemo wakuu wa nchi, mawaziri, na maafisa wakuu kutoka mashirika ya kimataifa.

Zaidi ya wakuu 20 wa nchi, manaibu 15, na zaidi ya mawaziri 50 wa mambo ya nje wanatarajiwa kushiriki, kwa mujibu wa vyanzo vya Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki.

Kwa jumla, jukwaa linatarajiwa kuwaleta pamoja zaidi ya washiriki 460 wa ngazi ya juu, ikiwa ni pamoja na takriban wawakilishi 75 kutoka mashirika ya kimataifa, sambamba na karibu wageni 5,000.

ADF26 itakuwa na uwakilishi wa kijiografia mpana, ambapo takriban nusu ya wakuu wa nchi wanaoshiriki watatoka Afrika na Ulaya.

Miongoni mwa mawaziri wa mambo ya nje, 40% watatoka Afrika, 35% Ulaya, na 22% Asia, kwa mujibu wa vyanzo.

Vikao vingi vitajadili masuala ya kimataifa

Programu itajumuisha zaidi ya vikao 40 na majukwaa ya ngazi ya viongozi, ikijikita katika mabadiliko ya kimataifa, kutokuwa na uhakika na mabadiliko ya mienendo ya kikanda.

Majadiliano pia yatazungumzia changamoto kubwa za kisiasa, kiuchumi, kimazingira, na teknolojia zinazounda mpangilio wa kidunia unaoendelea kubadilika.

Matukio ya pembeni yatazingatia masuala yakiwemo Jukwaa la Amani la Balkani, Gaza, Nchi za Turkiki, na mkutano wa pande nne kati ya Uturuki, Pakistan, Saudi Arabia, na Misri.