| Swahili
Maoni
MAISHA
8 dk kusoma
Nani anapaswa kuwajibika kwa madhara yanayosababishwa na matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto?
Katika nchi mbalimbali kuanzia Uturuki hadi Australia, mabadiliko mapya ya kisheria yanaonyesha mtazamo wa pamoja kwamba uangalizi wa wazazi pekee hauwezi kuzuia madhara ya mitandao ya kijamii kwa watoto.
Nani anapaswa kuwajibika kwa madhara yanayosababishwa na matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto?
Ulimwenguni kote, serikali huchukua hatua kudhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto. / AP / AP
4 Februari 2026

Msukumo wa kimataifa wa kudhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto unaondoa mzigo wa uwajibikaji kutoka kwa wazazi pekee na kuuelekeza zaidi kwa majukwaa ya kidijitali yanayoundwa ili kunufaika na kuvutia umakini wa watoto.

Duniani kote, serikali zinapochukua hatua za kudhibiti matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto, mjadala kuhusu madhara ya kidijitali unapitia mabadiliko ya msingi.

Kuanzia Australia hadi Uingereza, na kutoka Norway hadi Uturuki, kanuni zinazoandaliwa katika nchi nyingi zinakubaliana juu ya hoja moja kuu: madhara yanayosababishwa na matumizi ya mitandao ya kijamii kwa watoto hayawezi kuzuiwa kwa uangalizi wa wazazi pekee.

Uwajibikaji lazima ugawanywe pamoja na majukwaa ya kidijitali yanayobuni, kusimamia, na kunufaika kifedha na mazingira ya mtandaoni.

Mabadiliko haya hayaondoi jukumu la wazazi au mamlaka za umma. Familia na serikali bado ni wadau muhimu katika ulinzi wa watoto.

Hata hivyo, serikali sasa zinachukua msimamo ulio wazi zaidi na mkali zaidi kwamba uwajibikaji unapaswa kupanuliwa kwa majukwaa yanayobuni, kuboresha, na zinazofaidi kibiashara kutumia mazingira ya kidijitali.

Kama ilivyo kwa watumiaji wengine, watoto hawatumii tu mitandao ya kijamii; wanaelekezwa, kuhimizwa, na kushikiliwa kwenye majukwaa kupitia miundombinu iliyoboreshwa kwa ajili ya kuongeza faida.

Mifumo ya kusogeza skrini bila kikomo (infinite scrolling), mapendekezo ya kialgorithimu, na mifumo ya zawadi imeundwa kwa makusudi kudumisha uchumi.

Katika mazingira haya, kutarajia wazazi wawe nguvu pekee ya kupambana na mifumo ya kiuchumi yenye thamani ya trilioni za dola si jambo la kweli wala la haki.

Utafiti mkubwa wa kitaaluma kutoka taaluma mbalimbali kuhusu watoto na vijana unaonyesha kuwa matumizi kupita kiasi ya mitandao ya kijamii yanahusishwa kwa karibu na matatizo ya wasiwasi, unyogovu, matatizo ya usingizi, upungufu wa umakini, mtazamo potofu wa mwili unaochochewa na picha zilizochujwa, pamoja na matatizo ya ulaji.

Kufaidi kupitia data ya watumiaji

Dhana ya “kufaidi kupitia data” ya Shoshana Zuboff inatoa mfumo thabiti wa kuelewa kwa nini uwajibikaji inachukuliwa kwa umuhimu zaidi.

Majukwaa ya mitandao ya kijamii hukusanya na kuchambua tabia za watumiaji, hutabiri vitendo vyao vya baadaye, na hubadilisha taarifa hizi kuwa faida kupitia matangazo yanayolengwa na uelekezwaji wa tabia.

Katika mfumo huu, watoto si watumiaji dhaifu tu bali pia ni vyanzo muhimu vya data.

Kila kusogeza skrini, kupenda maudhui, na mwitikio wa kihisia huchangia katika kuunda tabia fulani.

Kwa watoto ambao ukuaji wao wa kiakili na kihisia bado unaendelea, uchunguzaji huu wa data una athari za kina na za muda mrefu zaidi.

Algorithimu hazijifunzi tu watoto wanachopenda; pia zinaunda kile watakachokuja kukitamani.

Kwa sababu hii, kanuni za sasa zinazidi kulenga kuweka mipaka ya ukusanyaji wa data za watoto, kupiga marufuku matangazo yanayolenga watumiaji fulani, kudai uwazi katika mifumo ya mapendekezo, na kuadhibu miundo inayoongeza matumizi kupita kiasi.

Ubepari wa kiteknolojia (Technofeudalism)

Wazo la Yanis Varoufakis la “teknofeudalismi” linatoa mtazamo wa ziada wa kuelewa ukosefu wa usawa wa nguvu.

Watumiaji hawamiliki maeneo haya ya kidijitali; wanapewa tu ruhusa ya kutumia kwa masharti yanayoamuliwa upande mmoja na wamiliki wa majukwaa.

Watoto hukua ndani ya mifumo hii binafsi ya utawala.

Malezi yao ya kijamii, muda wao wa burudani, na kwa kiwango kinachoongezeka, elimu yao, huundwa ndani ya mifumo isiyo wazi inayodhibitiwa na algorithimu badala ya usimamizi wa kidemokrasia.

Katika muktadha huu, mamlaka ya wazazi huwa dhaifu kimuundo katika kushindana na mamlaka ya kialgorithimu ambayo ni endelevu, isiyoonekana, na inayoweza kupanuka kwa kiwango kikubwa.

Kwa mtazamo huu, kuwalaumu wazazi ni pekee haitoshi ni lazima kuwawajibisha watoaji huduma hizo.

Serikali zinazotambua ukosefu huu wa usawa wa nguvu zinazidi kuhamisha mwelekeo wao kutoka kwa “raia” kwenda kwa “mabepari”.

Marufuku ya Australia ya matumizi ya mitandao ya kijamii kwa walio chini ya miaka 16, iliyoanza kutekelezwa tarehe 10 Disemba 2025, ni mojawapo ya mifano iliyo wazi zaidi ya mabadiliko haya.

Kwa baadhi ya mifumo michache kama YouTube Kids, majukwaa yanatakiwa kutekeleza mifumo madhubuti ya uthibitishaji wa umri; kushindwa kufanya hivyo kunasababisha kutozwa kwa faini ya hadi dola milioni 32.

Kauli ya aliyekuwa mtendaji wa Meta, Stephen Scheeler, kwamba kampuni hiyo inaweza kupata kiasi hicho kwa chini ya saa mbili, imezua maswali makubwa kuhusu uwezo wa adhabu hizi kuzuia ukiukaji.

Nchini Uingereza, Sheria ya Usalama Mtandaoni (Online Safety Act) inaipa Ofcom mamlaka ya kutoza makampuni faini hadi asilimia 10 ya mapato yao ya kimataifa.

Waziri Mkuu Keir Starmer, pamoja na wanasiasa wengine wengi, ameeleza wazi kuwa muda mwingi wa kutumia skrini unatishia ustawi wa watoto.

Maamuzi ya Bunge la Ulaya kuweka umri wa chini wa miaka 16 kwa matumizi ya mitandao ya kijamii na miaka 13 kwa zana za akili mnemba na majukwaa ya video pia yanaakisi mwelekeo huu.

Wakati Ufaransa ikijadili marufuku kamili kwa walio chini ya miaka 15 na aina ya “amri ya kutotumia dijitali usiku,” Hispania inaandaa kanuni zitakazohitaji idhini ya wazazi kwa watumiaji walio chini ya miaka 16.

Norway, kwa upande wake, imetambua kutofanya kazi kwa vikwazo vya sasa na inaendeleza mifumo madhubuti zaidi ya usimamizi.

Nchini Marekani, kizingiti cha umri cha miaka 13 kinacholenga faragha ya data bado kipo, lakini vikwazo vikali zaidi vya majimbo vinakabiliwa na changamoto za kisheria kuhusu uhuru wa kujieleza.

China inatekeleza mojawapo ya udhibiti mkali zaidi wa kidijitali kwa watoto.

Watoto walio chini ya miaka 14 wanaruhusiwa dakika 40 tu kwa siku za matumizi ya skrini, na matumizi ya kidijitali yanapigwa marufuku kabisa kati ya saa 4 usiku (10:00 p.m.) na saa 12 asubuhi (6:00 a.m.) kwa saa za eneo.

Ingawa TikTok ina zaidi ya watumiaji nusu bilioni duniani, nchini China inafanya kazi kupitia toleo tofauti linaloitwa Douyin, lenye algorithimu tofauti na msisitizo mkubwa juu ya maudhui ya kielimu.

Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron amesema wazi kuwa wakati China inaruhusu TikTok kudhoofisha umakini wa watoto duniani, inawaongoza watoto wake kupitia Douyin kwa maudhui yaliyo na nidhamu na elimu zaidi.

Tofauti hii inaonyesha kuwa mitandao ya kijamii haifanyi kazi tu kama taasisi za kibiashara bali pia kama njia ya upotoshaji wa kitamaduni.

Ukweli kwamba majukwaa ya Magharibi yamepigwa marufuku nchini China unaonyesha zaidi kuwa serikali zinazidi kuyaona majukwaa ya kidijitali si kama wahusika wa soko huria, bali kama miundombinu ya kimkakati.

Makampuni makubwa ya teknolojia na ‘‘kubadilisha maadili”

Ingawa makampuni makubwa ya teknolojia—yanayojulikana kama Big Tech—yametekeleza baadhi ya hatua hizi, bado kwa ujumla yanapinga vikwazo hivyo.

Baada ya kuanzishwa kwa marufuku hiyo, Waziri Mkuu wa Australia Anthony Albanese alisema kuwa zaidi ya akaunti milioni 4.7 za mitandao ya kijamii za watumiaji walio chini ya miaka 16 zilifutwa, kuzimwa, au kuwekewa vikwazo.

Wawakilishi wa Big Tech wanadai kuwa teknolojia za kuthibitisha umri zinahatarisha faragha, zinakiuka haki za watoto, na zinaweza hata kupunguza usalama mtandaoni.

Hata hivyo, pingamizi hizi mara nyingi huficha hofu ya kina zaidi: kupoteza kundi la watumiaji lenye faida kubwa sana linalozalisha data na maudhui bila malipo.

Mkurugenzi Mtendaji wa Meta Mark Zuckerberg, mkuu wa Instagram Adam Mosseri, na Mkurugenzi Mtendaji wa Snapchat Evan Spiegel wanatarajiwa kufikishwa mahakamani katika kesi zinazodai kuwa walibuni maudhui zenye kuzidisha uzoefu mbaya licha ya ushahidi wa madhara kwa watumiaji wachanga.

Wakati huohuo, ahadi za hiari kuhusu maadili na usalama zinazidi kufanana na kile kinachoweza kuitwa “kudhoofisha maadili”: kusambaza uwajibikaji bila kubadili mifumo ya msingi ya kibiashara.

Sera za ulinzi wa watoto nchini Uturuki

Mijadala kuhusu uwepo wa watoto katika mazingira ya kidijitali nchini Uturuki inaakisi hisia za ndani lakini kwa kiasi kikubwa inaendana na mwelekeo wa kimataifa wa udhibiti.

Rasimu ya ripoti yenye kichwa “Vitisho na Hatari Zinazowasubiri Watoto Wetu katika Mazingira ya Kidijitali”, iliyoandaliwa na Kamati Ndogo ya Haki za Mtoto ya Tume ya Uchunguzi wa Haki za Binadamu ya Bunge la Uturuki, inaeleza mfumo wa mtazamo huu.

Ripoti hiyo inapendekeza vikwazo vya matumizi ya usiku kwa walio chini ya miaka 18, marufuku ya mitandao ya kijamii kwa walio chini ya miaka 15, mipaka ya matumizi ya vifaa vya kidijitali shuleni, kuimarisha huduma za ushauri nasaha, na matumizi ya SIM kadi maalum kwa watoto.

Waziri wa Familia na Huduma za Jamii, Mahinur Ozdemir Goktas, ametangaza kuwa maandalizi ya kisheria kwa ajili ya udhibiti wa mitandao ya kijamii kwa watoto walio chini ya miaka 15 yatawasilishwa bungeni hivi karibuni.

Sababu za udhibiti huo ni pamoja na kuongezeka kwa unyogovu, wasiwasi, matatizo ya tabia, na hatari ya watoto kuwasiliana na mitandao ya uhalifu kupitia majukwaa ya kidijitali.

Waziri Goktas amesema wazi kuwa watoto hawatatendewa kama rasilimali za kibiashara au vyanzo vya data na majukwaa ya mitandao ya kijamii.

Badala ya kuwa kizuizi cha uhuru wa kujieleza, hatua hizi zinaelezwa kama sera ya kimkakati ya umma ya kulinda watoto dhidi ya hatari za kimuundo za mfumo wa kidijitali.

Katika muktadha huu, jukwaa la kidijitali la “Çocuklar Güvende” (Watoto Wako Salama) linatoa mwongozo na mifumo ya kutoa taarifa kwa watoto na wazazi.

Mamlaka zinasisitiza hasa kwamba mapambano dhidi ya maudhui hatarishi lazima yawe ya kinga na yaendeshwe na majukwaa yenyewe, badala ya kutegemea hatua za baadae pekee.

Watoto si kundi pekee linalokumbwa na madhara ya kidijitali.

Watu wazima wenye ujuzi mdogo wa kidijitali—hasa wazee—wanazidi kuwa hatarini kwa upotoshaji wa taarifa, mgawanyiko wa kihisia, na mbinu za udhibiti wa tabia zinazoendeshwa na algorithimu.

Kwa hiyo, udhibiti wa majukwaa si hatua ya kielimu ya kulinda watoto pekee.

Pia ni jitihada za kuimarisha mazingira ya umma ya kidijitali dhidi ya upotoshaji wa taarifa, kuzikomboa michakato ya kidemokrasia kutoka kwa udhibiti wa kialgorithimu, na kulinda mshikamano wa kijamii.

Ikiwa majukwaa yanabuni mazingira ya kidijitali, yanafundisha algorithimu, na yanapata faida kwa utaratibu kupitia uchumi wa umakini, basi uwajibikaji hauwezi kuwekwa kwa watu binafsi, familia, au mapendeleo ya watumiaji pekee.

Uwajibikaji lazima ugawanywe, na mamlaka lazima yawekwe chini ya usimamizi wa umma.

 

 

 

 

 

 

 

CHANZO:TRT World