Saka asaidia kujenga kijiji kwa waathirika wa poromoko la ardhi Morocco
Mchezaji wa Arsenal Bukayo Saka amejitolea kuwasaidia wahanga wa tetemeko la ardhi Morocco kwa kujenga kijiji cha makontena yatakayotoa makazi kwa familia 84, pamoja na watoto 89.
Winga matata wa viongozi wa ligi kuu ya Uingereza, Arsenal na England mwenye umri wa miaka 22 alichangia makontena 50 kwa jamii katika eneo la Taroudant, ili kutoa makazi kwa watu 255.
Miongoni mwa maeneo yaliyoathiriwa sana na tetemeko la ardhi yalikuwa Al Haouz, Taroudant, Chichaoua, Marrakech, Ouarzazate, Youssoufia, Tinghir, Azilal, na Agadir.
Mchango huo kutoka Saka alioufanya kupitia Shirika la Misaada ya Matibabu kwa watoto BigShoe, umewanufaisha wakazi wa kijiji kilichowapoteza kati ya watu 3,000 waliofariki katika msiba huo.
"Shukrani Kwa Bukayo Saka, sasa watoto wanapokea msaada, wana paa juu ya vichwa vyao tena na tabasamu kwenye nyuso zao," BigShoe ilisema katika chapisho lake.
Kwa upande wake, Saka alisema, "Natumai kuwa familia 84 na, zaidi ya yote, watoto 89 kwenye vyombo wanaweza kupata tena kipande cha maisha yao ya kila siku."
Msaada huo sio wa kwanza kutoka Saka, kwani mapema mwaka huu, mchezaji huyo wa Arsenal, kupitia ushirikiano na shirika hilo la BigShoe, aliweza kufanikisha ujenzi wa makazi kwa ajili ya waathirika wa tetemeko la ardhi nchini Uturuki.
Aidha, Saka pia alisaidia kutoa upasuaji wa kubadilisha maisha ya watoto 120 nchini Nigeria. "Katika hali ambapo watu wanapigania kuishi, kupoteza nyumba zao au wapendwa wao, unafahamu zaidi hali ya upendeleo unayoishi," mchezaji huyo alisema.