Hospitali za Gaza kusitisha huduma saa 48 zijazo, Wizara ya afya yasema

Mashambulizi ya Israeli dhidi ya Gaza yameingia siku ya 268, yakiwa yameua Wapalestina 37,877, wengi wakiwa ni wanawake na watoto, na kujeruhi wengine 86,969, huku zaidi ya 10,000 wakihofiwa kufunikwa na vifusi vya nyumba.

By Edward Josaphat Qorro
Kulingana na Wizara ya Afya, hali hiyo inatokana na upungufu mkubwa wa mafuta kwa ajili ya kufua umeme wa majenereta. / Picha: AA   / Others

Wizara ya Afya ya Gaza imetoa tahadhari kuwa huduma za afya katika eneo hilo huenda zikaathirika ndani ya saa 48 zijazo kutokana na upungufu mkubwa wa mafuta, kufuatia mashambulizi ya Israeli.

Katika taarifa yake, Wizara hiyo ilionya kuwa "hospitali na vituo vya afya vilivyobaki vitaacha kutoa huduma ndani ya saa 48.”

Wizara hiyo ilibainisha kuwa hali hiyo inatokana na "upungufu mkubwa wa mafuta ya kusaidia majenereta kufua umeme, ambayo pia "yamezuiwa kuingia Gaza na Israeli pamoja na huduma zingine za muhimu kama vile vyakula na madawa."

Wizara hiyo ilionyesha kuwa usambazaji wa mafuta unakaribia kuisha, "licha ya hatua kali za kubana matumizi zinazotekelezwa na wizara kuhifadhi akiba iliyobaki kwa muda mrefu iwezekanavyo, kutokana na kiasi cha kutosha kinachopatikana kwa uendeshaji."

Pata habari zaidi kupitia Whatsapp channels