Uganda inajiandaa kumruhusu mgongwa wa mwisho wa Ebola Julai 16, ikiashiria mwanzo wa kuhesabu siku 42 kabla ya nchi hiyo kutangazwa rasmi kutokuwa na maambukizi ya virusi, msemaji wa serikali amesema.
Kwa mujibu wa muongozo wa Shirika la Afya Duniani (WHO), nchi inaweza kutangazwa kuwa huru na maambukizi ya Ebola iwapo hakutakuwa na maambukizi mapya katika kipindi cha siku 42 mfululizo, baada ya mgonjwa wa mwisho kupona na kuruhusiwa.
Mwisho wa mlipuko Uganda
Wizara ya Afya ya Uganda imesema wagonjwa 17 wamepona, huku mmoja akiendelea kuwa karantini na vifo viwili kuthibitishwa.
Wizara imesema kuwa maambukizi ya wagonjwa watano yametoka ndani na 15 ni kutoka nje.
Msemaji wa Serikali Alan Kasujja amesema mgonjwa wa mwisho ataruhusiwa kutoka Hospitali ya Taifa ya Rufaa ya Mulago iliyopo jijini Kampala.
"Hilo litakapotokea, Uganda itaanza kuhesabu siku," ameandika Kasujja katika mtandao wa X.
"Iwapo siku 42 zitapita bila maambukizi mapya, muongozo wa WHO unasema tutatangazwa kuwa nchi isiyo na maambukizi ya Ebola."
Kutokana na mlipuko huo, WHO ilitangaza dharura ya afya ya umma katika Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo mwezi Mei, ambapo mlipuko huo ulisababisha maambukizi 2,011 na vifo 754 mpaka kufikia Jumatano, kwa mujibu wa taarifa za serikali ya nchi hiyo.
Maambukizi yote yaliyothibitishwa yamehusishwa na kirusi adimu aina ya Bundibugyo, ambacho WHO imeeleza kuwa ni mlipuko mkubwa wa tatu wa aina yake.














