| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Mfalme Oyo Nyimba kuzikwa leo kwa mujibu wa mila na desturi
Viongozi wa ukoo wa kifalme wamemchagua binamu yake Oyo, Edward Rukidi Kijanangoma, kuwa mfalme mpya.
Mfalme Oyo Nyimba kuzikwa leo kwa mujibu wa mila na desturi
Utawala wake ulidumu kwa zaidi ya miongo mitatu, jambo lililomfanya kuwa mtu muhimu katika uongozi wa kimila wa kisasa nchini Uganda.

Mfalme wa Uganda, Oyo Nyimba Kabamba Iguru Rukidi wa Nne, atazikwa leo katika mji wa Fort Portal ulioko magharibi mwa nchi hiyo, siku chache baada ya kufariki dunia akiwa na umri wa miaka 32.

Mfalme huyo wa Tooro, ambaye aliingia madarakani akiwa na umri wa miaka mitatu tu, anazikwa katika makaburi ya kifalme kufuatia ibada ya mazishi iliyofanyika katika Kanisa Kuu la St. John.

Kifo chake kimefuatiwa na mzozo usio wa kawaida kuhusu mrithi wa kiti cha ufalme.

Viongozi wa ukoo wa kifalme wamemchagua binamu yake Oyo, Edward Rukidi Kijanangoma, kuwa mfalme mpya.

Hata hivyo, mama na dada yake Oyo wamepinga uamuzi huo, wakisema kuwa marehemu mfalme alikuwa amemteua mtu mwingine kuwa mrithi wake.

Mzozo huo umeongeza hali ya taharuki katika sherehe hiyo ambayo tayari ilikuwa imejaa hisia nzito, huku ulinzi ukiimarishwa zaidi katika eneo la Fort Portal.

Kwa mujibu wa mila za Tooro, mfalme mpya lazima atekeleze tambiko muhimu wakati wa mazishi, ikiwa ni pamoja na kutupa punje tisa za kahawa kaburini, kama ishara ya mabadiliko na utambuzi wa mfalme mpya, ingawa sherehe rasmi ya kumtawaza mbele ya umma bado haijafanyika.

Oyo alikuwa mmoja wa wafalme wadogo zaidi duniani aliporithi kiti cha ufalme wa Tooro mwaka 1995.

Utawala wake ulidumu kwa zaidi ya miongo mitatu, jambo lililomfanya kuwa mtu muhimu katika uongozi wa kimila wa kisasa nchini Uganda.

Uganda inaongozwa na mkuu wa nchi aliyechaguliwa, lakini bado ina falme kadhaa zilizokuwepo kabla ya enzi ya ukoloni wa Uingereza na ambazo huchukuliwa kuwa nguzo za utambulisho na urithi wa kimila.

CHANZO:TRT Afrika Swahili