Ndege ya kwanza ya kuwaondoa raia wa Ghana waliokuwa nchini Afrika Kusini kufuatia vitisho dhidi ya wageni iliondoka Jumatano kuelekea mjini Accra, kwa mujibu wa Wizara ya Mambo ya Nje ya nchi hiyo.
Raia wa Ghana wapatao 800 wanatarajiwa kuondoka Afrika Kusini baada ya Ghana kuratibu ndege za kuwarudisha nyumbani raia wake ambao walikuwa Afrika Kusini. Hatua hii inafuatia maandamano na vitisho vilivyoelekezwa kwa raia wa kigeni wanaoishi nchini humo.
"Taarifa niliyokuwa nayo inaonesha kuwa ndege ilichelewa kuondoka, lakini hivi sasa iko njiani," Fred Duhoe, msaidizi wa Waziri wa Mambo ya Nje wa Ghana aliiambia AFP.
Mpiga picha wa AFP aliwaona mamia wa raia wa Ghana wakiwa katika foleni katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa O.R. Tambo, nje ya jiji la Johannesburg, Jumatano.
Kiwango cha ukosefu wa ajira
Mtandao wa kufuatilia safari za ndege FlightAware umeonesha ndege ikiondoka baada ya saa tano za asubuhi.
Balozi wa Ghana nchini Afrika Kusini amesema raia 300 wanatarajiwa kuondoka kwa ndege ya kwanza, ambayo ingefika siku ya Jumatano.
Serikali ya Ghana imeahidi kuwapa wale waliorudishwa kutoka Afrika Kusini msaada wa kifedha na kisaikolojia ili kuwasaidia kuanza maisha.
Afrika Kusini, ambayo ina kiwango cha asilimia 30 ya watu kukosa ajira, imeshuhudia maandamano ya mara kwa mara ya raia wake wakipinga uwepo kwa raia wa kigeni, kwa madai wanachukua ajira zao.
Wakati huo huo, serikali ya Afrika Kusini imewataka raia wake kuwa na utulivu na kuwakaribisha wageni ambao wanakidhi vigezo vya kuwepo nchini.
















