| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
Pentagon yasema vita vya Marekani dhidi ya Iran vimegharimu Dola bilioni 29 hadi sasa
Makadirio mapya ya Pentagon kuhusu gharama za vita vya Marekani yametangazwa huku gharama za Israel zikikadiriwa kuwa Dola bilioni 17.5 na Iran ambayo imepata hasara zinazokadiriwa kufikia Dola bilioni 270, inadai fidia katika mazungumzo na Marekani.
Pentagon yasema vita vya Marekani dhidi ya Iran vimegharimu Dola bilioni 29 hadi sasa
Marekani imetuma takriban wanajeshi zaidi ya 50,000 karibu na Iran. / / Reuters

Marekani imetumia thamani ya Dola bilioni 29 hadi sasa katika vita dhidi ya Iran, afisa mwandamizi wa Pentagon amesema, ikiwa ni ongezeko la Dola bilioni 4 kutoka makadirio yaliyotolewa mwishoni mwa mwezi uliopita.

Ikiwa zimebaki miezi sita kabla ya uchaguzi wa wabunge ambapo chama cha Republican cha Rais Donald Trump kinaweza kukumbana na changamoto kubwa ya kudumisha wingi wao katika Bunge, Wanademokrasia wanaendelea kufanya vizuri katika kura za maoni za umma huku wakijaribu kuhusisha vita hivyo na changamoto za gharama ya maisha.

Mnamo Aprili 29, Pentagon ilisema kuwa vita hivyo vilikuwa vimegharimu Dola bilioni 25 kufikia wakati huo.

Jules Hurst, anayetekeleza majukumu ya mdhibiti wa fedha, aliwaambia wabunge siku ya Jumanne kuwa gharama mpya zinajumuisha makadirio yaliyosasishwa ya ukarabati na uingizwaji wa vifaa pamoja na gharama za operesheni.

“Timu ya wafanyakazi wa pamoja na timu ya mdhibiti wa fedha wanaendelea kufuatilia makadirio hayo kila wakati,” alisema Hurst. Alikuwa akizungumza pamoja na Waziri wa Ulinzi Pete Hegseth na Mwenyekiti wa Wakuu wa Majeshi, Jenerali Dan Caine.

Haijulikani wazi jinsi Pentagon ilivyofikia kiwango hicho cha Dola bilioni 29.

Chanzo kiliiambia shirika la habari la Reuters mwezi Machi kwamba utawala wa Trump ulikadiria siku sita za kwanza za vita hivyo ziligharimu angalau Dola bilioni 11.3.

Hasara za Iran na Israel

Wizara ya Fedha ya Israel ilikadiria gharama ya siku 40 za vita dhidi ya Iran na Lebanon kuwa karibu dola bilioni 17.5, shirika la habari la Israel Channel 12 liliripoti mwezi uliopita.

Wakati wa vita hivyo, Iran ilirusha takriban makombora 650 ya balestiki kuelekea Israel, yakisababisha uharibifu mkubwa na vifo vya watu, kwa mujibu wa vyombo vya habari vya Israel.

Maafisa wa Iran wamekadiria hasara za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja katika vita hivyo kuwa karibu dola bilioni 270. Kiwango hicho kinajumuisha uharibifu wa miundombinu na hasara za kiuchumi, na Iran imedai fidia katika mazungumzo na Marekani.

Marekani iliungana na Israel katika kuishambulia Iran mnamo Februari 28, huku mashambulizi yakisababisha kifo cha kiongozi mkuu wa muda mrefu, Ali Khamenei, pamoja na viongozi wengine wengi wa ngazi ya juu, wakiwemo mamia ya raia.

Lakini Iran ilijibu haraka kwa kudhibiti Mlango-Bahari wa Hormuz, njia muhimu ya kupitisha asilimia 30 ya mafuta duniani. Irana imeendelea kurusha makombora na ndege zisizo na rubani dhidi ya nchi za Ghuba zinazoshirikiana na Marekani, jambo lililovunja sifa ya uthabiti ambayo nchi hizo tajiri wa mafuta zilikuwa zimeijenga kwa muda mrefu.

Huku usitishaji vita dhaifu uliosimamiwa na Pakistan tangu Aprili 8 ukiendelea, Rais wa Marekani amepuuza kwa hasira majibu ya hivi karibuni ya Iran kuhusu pendekezo la Marekani la suluhu, akionya kuwa makubaliano hayo ya kusitisha vita yako katika hali tete sana.

CHANZO:TRT World and Agencies