| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Polisi nchini Kenya wafukua zaidi ya miili 33 katika kaburi la pamoja
Mamlaka katika magharibi mwa Kenya ilisema siku ya Alhamisi kuwa imefukua angalau miili 33 kutoka katika kaburi la pamoja, na mabaki ya miili hiyo inaaminika kutoka katika vyumba vya kuhifadhi maiti.
Polisi nchini Kenya wafukua zaidi ya miili 33 katika kaburi la pamoja
Polisi nchini Kenya wamefukua miili 33 kutoka kwenye kaburi la pamoja katika mji wa Kericho, magharibi mwa nchi hiyo. / / AP
tokea masaa 4

Maafisa wa upelelezi wa mauaji walifukua mabaki ya miili ya watu wazima wanane na watoto 25, pamoja na vipande vya miili vilivyokatwakatwa na kufungwa kwenye magunia katika kaburi la pamoja katika eneo la makaburi linalomilikiwa na kanisa moja mjini Kericho, magharibi mwa Kenya.

“Tuliweza kubaini kuwa hii ilikuwa miili iliyohamishwa kutoka Hospitali ya Wilaya ya Nyamira na kuzikwa katika makaburi ya kibinafsi huko Kericho,” alisema Mohamed Amin, mkuu wa Idara ya Upelelezi wa Jinai, akizungumza na waandishi wa habari.

Amin alisema wapelelezi wanataka kubaini kama miili hiyo ilizikwa kwa njia halali baada ya kuondolewa kutoka chumba cha kuhifadhi maiti.

Watu wawili wakamatwa

Chini ya sheria za Kenya, hospitali na vyumba vya kuhifadhi maiti vinatakiwa kuondoa miili ambayo haijachukuliwa na wenye maiti kwa zaidi ya siku 14. Mchakato huo unahitaji idhini ya amri ya mahakama.

Madaktari wa serikali walifanya uchunguzi wa miili hiyo siku ya Alhamisi ili kubaini chanzo cha vifo. Hadi sasa hakuna taarifa rasmi kuhusu majina au waliozikwa makaburini humo.

Angalau watu wawili wamekamatwa.

Vyombo vya habari vya ndani viliripoti kuwa watu wasiojulikana walileta miili hiyo kutoka sehemu nyingine na kuizika kwa haraka. Inasemekana baadhi ya wachimbaji makaburi waliiarifu polisi.

Matukio mengine kama hayo

“Tunahitaji mamlaka kufanya uchunguzi wa kina,” alisema mkazi Brian Kibunja.

Hili ni tukio la tatu kubwa la makaburi ya pamoja nchini Kenya katika kipindi cha miaka mitatu iliyopita.

Mnamo 2023, polisi waligundua mamia ya miili iliyozikwa katika msitu katika eneo la pwani la Kilifi nchini Kenya. Miili hiyo ilifukuliwa kutoka makaburi ya pamoja yaliyohusishwa na kiongozi wa kidini aliyewanyima wafuasi wake chakula hadi kufa.

Mnamo 2024, mamlaka ilipata miili tisa kutoka dampo la taka jijini Nairobi, mji mkuu.