| Swahili
ULIMWENGU
2 dk kusoma
Urusi yaishukuru Uturuki kwa utayari wake wa kusaidia mchakato wa amani Ukraine
Msemaji wa Kremlin amesema migogoro mingi ni "tata sana", na kujaribu kuisuluhisha kupitia "makubaliano" kunaweza kuwa jambo "lisilowezekana."
Urusi yaishukuru Uturuki kwa utayari wake wa kusaidia mchakato wa amani Ukraine
Msemaji wa Kremlin alizungumzia yanayojiri Ukraine, ameisema mabadiliko katika serikali hayana umuhimu wa msingi kwa Urusi. / / Reuters

Msemaji wa Kremlin, Dmitry Peskov, amesema kuwa Urusi inaishukuru Uturuki kwa utayari wake wa kuwezesha mchakato wa kupatikana kwa suluhu kuhusu mzozo wa Ukraine.

"Tunafahamu vyema utayari wa marafiki zetu wa Uturuki wa kuendelea kuwezesha suluhu ya amani ya hali iliyopo nchini Ukraine. Tunaishukuru upande wa Uturuki kwa hili," msemaji wa Kremlin, aliwaambia waandishi wa habari katika mkutano wa Alhamisi.

Alisema kuwa Urusi haioni matarajio ya haraka ya kuanza tena mazungumzo kuhusu mzozo huo, lakini bado iko tayari kushiriki katika mazungumzo.

Uturuki iliandaa mazungumzo ya amani kati ya Urusi na Ukraine mjini Istanbul katika majira ya kiangazi ya mwaka 2025, huku duru tatu za mazungumzo zikifanyika mwaka huu jijini Abu Dhabi na Geneva. Hata hivyo, mazungumzo hayo yamesitishwa tangu vita vya Iran.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Uturuki, Hakan Fidan, alisema jijini Kyiv siku ya Alhamisi kwamba kuanzishwa tena kwa mchakato wa Istanbul kutaleta manufaa.

Peskov alieleza kuwa migogoro mingi huwa na "muundo tete sana", na kwamba kuisuluhisha kupitia "makubaliano", akiashiria pendekezo la Marekani, linaweza kuwa jambo "lisilowezekana."

"Inahitaji mchakato mrefu, changamani na wa kina wa kutafuta suluhu. Hii ndiyo njia pekee ya kufikia utatuzi," alisema Peskov.

Pia aliepuka kulinganisha au kuweka uhusiano kati ya hali ya Ukraine na Iran, akisema: "Kila mzozo unatofautiana na mwingine na kwa mambo mahususi yanayopaswa kushughulikiwa katika mchakato wa kuutatua.”

Akizungumzia Iran, Peskov alisema kuwa Urusi, kama nchi nyingine, imeeleza wasiwasi wake kuhusu ongezeko jipya la hali ya kuyumba katika eneo la Ghuba.

"Haya yote yanaweza kusababisha kuendelea kwa madhara hasi kwa uchumi wa dunia, jambo ambalo haliwezi kukosa kuleta wasiwasi," alisema Peskov, huku akielezea hali ya uchumi wa dunia kuwa "mbaya kwa kiasi kikubwa."

Msemaji huyo pia alizungumzia yanayojiri nchini Ukraine, akisema mabadiliko katika serikali hayana umuhimu wa msingi kwa Urusi.

"Kilicho muhimu kwetu ni kutatua hali hiyo na kuhakikisha maslahi yetu wenyewe," alisema Peskov, huku akikiri kwamba Urusi inafuatilia taarifa zote zinazohusiana na Kyiv.

Siku ya Jumapili, Rais wa Ukraine, Volodymyr Zelenskyy, alitangaza mabadiliko katika Baraza la Mawaziri, na waziri mkuu mpya, mkurugenzi wa sekta ya nishati Serhii Koretskyi, aliidhinishwa na bunge siku ya Alhamisi.