Brigedia Ali Rizqallah, maarufu Savanah, amesema katika video iliyosambaa mitandaoni Jumatatu kwamba "amejiunga na utashi wa watu wa Sudan."
"Kuanzia leo, tuko upande mmoja na RSF iko upande mwengine. Sauti yangu ni sauti ya watu wa Sudan katika mikoa yote, mashariki, magharibi, kusini, na kaskazini. Sauti yangu ni sauti ya wakimbizi na waliokosa makazi," alisema.
Hakuna kauli iliyotolewa na RSF kuhusu kujitoa kwa brigedia huyo.
Savanah alikuwa ni kamanda mwandamizi RSF, ambae aliongoza mapigano dhidi ya jeshi katika mji wa Khartoum na El Fasher, mji mkuu wa jimbo la North Darfur.
Mpaka sasa hakuna taarifa ya kikosi anachokiongoza.
Huyu ni kiongozi wa pili wa jeshi kujiondoa RSF tangu mwezi jana. Mwezi April, kamanda wa RSF Al-Nur Al-Qubba nae alijitoa na kujiunga na jeshi.
Sudan imekuwa katika mapigano ya wenyewe kwa wenyewe tangu Aprili 2023, kati ya vikosi vya RSF na jeshi, mapigano ambayo yamesababisha vifo vya maelfu, huku takriban milioni 13 wakikosa makazi, wengine wakikimbilia nchi jirani. Nchi hiyo hivi sasa inakabiliwa na ukame ambao umesababisha janga la kibinadamu kubwa zaidi kuwahi kutokea duniani.

















