| Swahili
AFRIKA
2 dk kusoma
Sierra Leone yakubali kupokea kundi la kwanza la wahamiaji wanaofukuzwa Marekani
Sierra Leone ni nchi ya hivi karibuni barani Afrika ambayo imeingia makubaliano kama hayo na Marekani, na itapokea ufadhili wa dola milioni 1.5 kusaidia mpango huo.
Sierra Leone yakubali kupokea kundi la kwanza la wahamiaji wanaofukuzwa Marekani
Rais Donald Trump amekuwa akiwaandama wahamiaji toka arudi madarakani kwa muhula wake wa pili. / / Reuters

Siku ya Jumatano, Sierra Leone itapokea kundi la kwanza la wahamiaji wanaorejeshwa kutoka Marekani, wakati serikali ya Rais Donald Trump ikiendelea na mpango wa kuwarudisha wahamiaji kwenda katika nchi zinazoendelea.

Waziri wa Mambo ya Nje wa Sierra Leone, Timothy Musa Kabba, alisema kuwa ndege ya kwanza itabeba wahamiaji 25 na itawasili katika mji mkuu Freetown Jumatano asubuhi. Hii ni sehemu ya makubaliano ya nchi hiyo kupokea hadi wahamiaji 300 kwa mwaka wenye asili ya Afrika Magharibi.

Sierra Leone inakuwa miongoni mwa nchi nyingine za Afrika ambazo zimekuwa na makubaliano kama hayo na Marekani, zikiwemo Cameroon, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Eswatini, Equatorial Guinea, Ghana, Rwanda na Sudan Kusini.

Waziri wa Mambo ya Nje huyo, alisema: “Tunawapokea wahamiaji kwa sababu wanatoka Afrika Magharibi, na baadhi wana nyaraka za Sierra Leone walizokuwa nazo miaka mingi iliyopita.”

Kipindi cha siku 90

Wahamiaji hao wataruhusiwa kukaa nchini kwa muda wa siku 90, na baadaye wanaweza kusafiri kurudi katika nchi zao za asili.

Marekani itatoa dola milioni 1.5 kusaidia gharama za kibinadamu na za uendeshaji wa mpango huo.

Kwa kawaida, nchi za Afrika zinazokubali kupokea wahamiaji wasio na hati kutoka Marekani hupata ufadhili wa Marekani kama sehemu ya makubaliano hayo. Baadhi ya nchi, kama ya DRC, zimekubali pia kupokea wahamiaji kutoka maeneo mengine kama Amerika ya Kusini.

CHANZO:AFP