Mwamuzi huyo wa Somalia Omar Artan aliyewahi kupata tuzo ameondolewa katika orodha ya waamuzi waliotakiwa kuwepo katika michuano ya mwanzo baada ya kuzuiwa kuingia Marekani, FIFA imesema Jumatatu.
Msemaji wa FIFA amethibitisha katika taarifa kwamba, Artan, ambae alikataliwa kuingia nchini Marekani baada ya kufika katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Miami Jumamosi, hatakuwa na jukumu lolote katika michuano ya Kombe la Dunia.
Iwapo angekubaliwa kuingia nchini Marekani, Artan angekuwa raia wa kwanza wa Somalia kuwa mwamuzi katika Kombe la Dunia.
"FIFA inathibitisha kwamba, Omar Abdulkadir Artan hataweza kupata mafunzo na kuwa mwamuzi katika Kombe la Dunia la 2026 baada ya kuzuiwa kuingia nchini Marekani," msemaji wa FIFA ameiambia AFP.
FIFA haina uwezo
FIFA imesisitiza kwamba haikuwa na uwezo wa kushawishi uamuzi, ambapo ilisema mamlaka hayo yanabaki kwa nchi mwenyeji Marekani.
"FIFA haihusiki na taratibu za uhamiaji za nchi mwenyeji, ikiwemo utoaji viza, na imeambiwa na mamlaka kwamba hali ya Bwana Artan haitabadilika kwa sasa," amesema msemaji.
"Kama ilivyo kwa matukio mengine ya FIFA, serikali wenyeji zinaamua nani apate viza na nani ataruhusiwa kuingia katika nchi yao."
Msemaji wa Forodha na Mipaka nchini Marekani (CBP) amesema Artan alizuiwa kufuatia ukaguzi wa kawaida.
"Baada ya ukaguzi, ilibainika kwamba msafiri ambae ni mwamuzi katika Kombe la Dunia la FIFA, asiruhusiwe hivyo kuzuiwa kuingia."
Marufuku ya Trump
Somalia ni miongoni mwa nchi kadhaa ambazo raia wake wamepigwa marufuku na serikali ya Donald Trump kuingia nchini humo kama sehemu ya msako wa idara ya uhamiaji.















