| Swahili
MICHEZO
3 dk kusoma
Algeria na Morocco zafuzu Kombe la Dunia la Wanawake
Algeria ilifuzu kwa mara ya kwanza kabisa kushiriki Kombe la Dunia la Wanawake, na itaungana na wapinzani wao kutoka Afrika Kaskazini, Morocco, katika fainali za 2027 nchini Brazil.
Algeria na Morocco zafuzu Kombe la Dunia la Wanawake
Algeria tayari imefuzu kwa Kombe la Dunia la Wanawake, ikiungana na jirani yake wa Afrika Kaskazini, Morocco. / reuters

Algeria imefanikiwa kufuzu kwa mara ya kwanza kabisa kushiriki Kombe la Dunia la Wanawake na itaungana na wapinzani wao wa Afrika Kaskazini, Morocco, katika fainali za mwaka ujao nchini Brazil, baada ya timu zote mbili kushinda mechi zao za robo fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake siku ya Jumamosi.

Algeria iliifunga Côte d'Ivoire, iliyokuwa ikicheza na wachezaji 10, kwa mabao 2-1 jijini Casablanca, huku Morocco ikiishinda Afrika Kusini kwa matokeo hayo hayo jijini Rabat na kuthibitisha nafasi yao baada ya hapo awali kushiriki Kombe la Dunia la 2023.

Timu nne zitakazofika nusu fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika zitafuzu kwa mashindano hayo ya dunia yatakayofanyika kuanzia Juni 24 hadi Julai 25 mwakani.

Côte d'Ivoire na Afrika Kusini bado zina nafasi ya kufuzu kupitia mechi za mchujo za mabara za FIFA, ambapo nafasi tatu za ziada za kushiriki Kombe la Dunia zinawaniwa.

Morocco itakabiliana na Cameroon au Nigeria

Timu hizo zitashiriki mechi za mchujo wakati wa Kombe la Mataifa ya Afrika siku ya Alhamisi ili kubaini ni nani atakayepata mojawapo ya nafasi mbili zilizotengwa kwa ajili ya Afrika katika mchujo wa mabara.

Katika hatua inayofuata, Morocco itakutana na mshindi wa robo fainali ya tatu kati ya Cameroon na Nigeria siku ya Jumapili, huku Algeria ikisubiri mshindi wa mechi kati ya Ghana na Malawi.

Afrika Kusini itakabiliana na timu itakayopoteza katika mchezo kati ya Cameroon na Nigeria kwenye mchujo wa mashindano ya mabara, huku Côte d'Ivoire ikikutana na ama Ghana au Malawi.

Mabao ya kipindi cha pili yaliyofungwa na Ines Khiri na Amira Ould Braham yalihitimisha ushindi wa Algeria katika robo fainali hiyo, baada ya timu hiyo kurejea mchezoni na kushinda licha ya kutanguliwa kufungwa bao na Ines Konan wa Côte d'Ivoire.

Kadi nyekundu

Timu hiyo ya Côte d'Ivoire ilimpoteza mchezaji hatari Nsira Ouedraogo, aliyeonyeshwa kadi nyekundu katika dakika ya 41 kwa kumpiga teke usoni kipa wa Algeria, Chloe N'Gazi; pia walikosa penalti katika kipindi cha pili ambapo Rebecca Elloh alipiga mpira uliogonga mwamba wakati matokeo yakiwa 1-1.

Morocco iliongoza kwa mabao 2-0 katika robo fainali yao kupitia kwa Sakina Ouzraoui na Hanane Ait El Haj (kwa penalti), lakini ilipata upinzani mkali baada ya Thembi Kgatlana kuifungia Afrika Kusini bao moja katikati ya kipindi cha pili.

Kumekuwa na washindi watatu pekee wa awali wa Kombe la Mataifa ya Wanawake. Nigeria ina rekodi ya mataji 10, ikifuatiwa na Guinea ya Ikweta yenye mataji mawili na Afrika Kusini yenye taji moja.

CHANZO:reuters