Serikali ya DRC kukutana na waasi wa M23, Aprili 9 nchini Qatar

Qatar imekuwa mwenyeji wa awamu ya pili ya mazungumzo kati ya nchi hizo yaliyoanza siku ya Ijumaa, huku ikikutana na wawakilishi wa M23.

Machi 18 mwaka huu, Rais wa DRC Felix Tshisekedi na Paul Kagame wa Rwanda, walikutana jijini Doha, mbele ya kiongozi wa nchi hiyo Sheikh Tamim bin Hamad Al-Thani./Picha: Wengine

Serikali ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) imepanga kufanya mazungumzo ya kwanza kabisa na kikundi cha waasi wa M23, April 9 mwaka huu, nchini Qatar, yenye nia ya kutafuta amani katika eneo la Mashariki mwa nchi hiyo.

Siku ya Jumanne, vyanzo kutoka pande zote mbili vilithibitisha uwepo wa mkutano unaotarajiwa kufanyika Aprili 9, 2025, jijini Doha.

Kikao hicho, kitakuwa cha kwanza kwa pande hizo toka waasi wa M23 wafanikiwe kudhibiti miji mikubwa miwili, mashariki mwa DRC.

Machafuko nchini DRC yamesababisha vifo vya maelfu ya watu, huku wengi wakilazimika kuyakimbia makazi yao.

 Mmoja wa maofisa kutoka serikali ya DRC, alisema kuwa kikao hicho kimepangwa kufanyika Aprili 9, huku upande wa M23 ukiweka wazi kuwa utapeleka masharti kwa serikali ya DRC.

Hata hivyo, pande zote mbili zimekubaliana kutoweka wazi ajenda za mkutano huo, vilisema vyanzo hivyo.

Machi 18 mwaka huu, Rais wa DRC Felix Tshisekedi na Paul Kagame wa Rwanda, walikutana jijini Doha, mbele ya kiongozi wa nchi hiyo Sheikh Tamim bin Hamad Al-Thani.

Qatar imekuwa mwenyeji wa awamu ya pili ya mazungumzo kati ya nchi hizo yaliyoanza siku ya Ijumaa, huku ikikutana na wawakilishi wa M23.