Idadi ya vifo katika shambulio la jimbo la Plateau la Nigeria yaongezeka hadi 28

Gavana wa jimbo la Plateau amethibitisha kuwa idadi ya vifo kutokana na mashambulizi ya watu wenye silaha katika jamii ya Angwan Rukuba Jos Kaskazini imeongezeka hadi 28.

By
Jimbo la Plateau nchini Nigeria limekumbwa na ukosefu wa usalama katika siku za hivi karibuni. / Reuters

Gavana wa jimbo la Plateau, Caleb Mutfwang, amethibitisha kuwa idadi ya waliouawa kutokana na mashambulizi ya watu wenye silaha eneo la Angwan Rukuba huko Jos Kaskazini imeongezeka hadi 28.

Katika taarifa kwa vyombo vya habari siku ya Jumanne, Mutfwang alieleza tukio hilo kama la "kikatili" na "baya," akiapa kuwa wale waliohusika watakamatwa na kuwajibishwa.

Shambulizi hilo lilitokea Jumapili usiku eneo la Angwan Rukuba huko Jos, ambapo waliwafyatulia wakazi risasi, na kuwaua kadhaa pamoja na kuwajeruhi wengine.

Awali serikali za mitaa zilitoa taarifa za idadi ndogo ya waliouawa kabla gavana kuthibitisha idadi hii ya sasa.

Maafisa wa usalama wamepelekwa

Mutfwang, ambaye aliwatembelea wakazi hao pamoja na wale waliojeruhiwa, alitoa salamu zake za rambirambi kwa familia za wale waliouawa na kuwahakikishia wakazi kuhusu dhamira ya serikali ya kurudisha amani na usalama.

Maafisa wa usalama wameagizwa kuimarisha operesheni katika eneo hilo ya kuwasaka waliohusika, aliongeza.

Hakuna kundi lililodai kuhusika na mashambulizi ya Angwan Rukuba.