Waziri wa Afya wa Zambia apigwa kalamu katika mabadiliko ya ghafla ya baraza la mawaziri

Hakainde Hichilema amesema watakaouchukua nafasi hizo watatangazwa kwa wakati muafaka.

By
Rais Hakainde Hichilema aliingia madarakani kama Rais wa 7 wa Zambia tarehe 24 Agosti 2021. / / AP

Rais wa Zambia, Hakainde Hichilema, alimfuta kazi Waziri wa Afya Elijah Muchima usiku wa Jumatano katika mabadiliko ya ghafla ya baraza la mawaziri.

Hichilema pia alimfuta kazi Waziri wa Kukuza Biashara Ndogo na za Kati, Elias Mubanga, huku Ikulu ikisema mabadiliko hayo yalifanywa kwa mujibu wa Ibara ya 116 (3) (a) ya Katiba ya Zambia.

“Rais amewasilisha shukrani zake kwa Mheshimiwa Muchima na Mheshimiwa Mubanga kwa huduma yao kwa Serikali ya Jamhuri ya Zambia na anawatakia kila la heri katika shughuli zao zijazo,” alisema Mkuu wa Mawasiliano wa Ikulu, Clayson Hamasaka, katika taarifa.

Elijah Muchima aliteuliwa kuwa Waziri wa Afya wa Zambia mwezi Julai 2024 katika mabadiliko ya baraza la mawaziri yaliyofanywa na Rais Hichilema. Alichukua nafasi hiyo kutoka kwa Sylvia Masebo kama sehemu ya upangaji upya wa serikali.

Hakuna sababu zilizotolewa kuhusu kufutwa kazi huko karibuni, huku Rais Hichilema akisema watakaochukua nafasi watatangazwa kwa wakati muafaka.