Rais wa Uturuki Recep Tayyip Erdogan amemlaki Waziri Mkuu wa Sudan Kamil Idris, ambaye yuko katika ziara ya kikazi nchini Uturuki, kwenye Ikulu ya Rais jijini Ankara, kulingana na Kurugenzi ya Mawasiliano ya Uturuki.
Mkutano huo wa Jumatano uliangazia uhusiano kati ya Uturuki na Sudan, pamoja na masuala ya kikanda na ulimwenguni, kurugenzi ilisema katika mtandao wa kijamii wa Uturuki NSosyal.
Erdogan amesema nchi hizo mbili zinalenga kuimarisha uhusiano kupitia hatua za sasa na zile za mustakabali, akisisitiza kuwa Uturuki itaendelea kuunga mkono uhuru wa Sudan na mipaka yake.
Rais wa Uturuki pia alisema kuwa Uturuki inajitahidi kusaidia katika kumaliza mapigano nchini Sudan na kurudisha hali kuwa ya kawaida, akiongeza kuwa Uturuki inaunga mkono juhudi za kidiplomasia kusitisha mapigano na kuanzisha mchakato kamili wa kisiasa.
Erdogan alieleza kuwa misaada inayolenga kuwapunguzia matatizo watu wa Sudan itaendelea katika kipindi hiki.
Mkutano huo pia ulihudhuriwa na Makamu wa Rais wa Uturuki Cevdet Yilmaz, Waziri wa Mambo ya Nje Hakan Fidan, Waziri wa Nishati na Maliasili Alparslan Bayraktar, Waziri wa Kilimo na Misitu Ibrahim Yumakli, na Mkurugenzi wa Mawasiliano Burhanettin Duran.



















