Kuna wagombea wanne wanaowania kumrithi Antonio Guterres ambaye anakamilisha muongo mmoja wa kuwepo kwenye nafasi hiyo.
Waliofika kwenye hatua hii ya mwisho ni Michelle Bachelet, Rebeca Grynspan, Rafael Grossi na Macky Sall.
Michelle Bachelet, Rais wa zamani wa taifa la Chile. Ni mwanamke pekee kuwahi kuongoza taifa hilo. Ana umri wa miaka 74 na amewahi kuhudumu katika mashirika tofauti ya Umoja wa Mataifa.
Alipendekezwa na Brazil, Mexico na Chile kwa pamoja.
Pamoja na kutokuwepo na mfumo rasmi wa mzunguko wa kimaeneo kuhusu uteuzi wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa, wengine wanaona ni zamu ya kanda ya Amerika ya Kusini.” “Mara ya mwisho kwa kanda kuwa na mtu kwenye nafasi hiyo ilikuwa miaka 35 iliopita,” mchambuzi wa masuala ya siasa Ovigwe Eguegu ameiambia TRT Afrika.
Mwingine ni Rafael Mariano Grossi Mwanadiplomasia wa Argentina ambaye amekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Kimataifa la Nishati ya Atomiki tangu 2019. Ana umri wa miaka 65 na ana utaalamu wa masuala ya nyuklia na usalama kimataifa.
Aliyekuwa Rais wa Senegal Macky Sall mwenye umri wa miaka 64 pia yuko katika kuwania nafasi hiyo akiwakilisha bara la Afrika. Ana uzoefu wa kisiasa katika kanda, na kuwa na nafasi muhimu ya upatanishi wa kidiplomasia.
Mgombea mwingine ni Rebeca Grynspan Mayufis, ambaye kwa sasa ni mkuu wa Shirika la Biashara na Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNCTAD).
Grynspan ambaye amewahi kuwa makamu wa rais wa taifa la Costa Rica ana umri wa miaka 70.
Wakati wa kuhojiwa, aliahidi kulipa kipaumbele suala la kutafuta amani. Alieleza kuhusu kuwahi kukabiliana na hali mapema, kufanya majadiliano ya moja kwa moja na kushirikiana kwa karibu na Baraza la Usalama, pamoja na mataifa wanachama 193 ya Umoja wa Mataifa.
“Nitakuwa mpatanishi wa amani. Nitafika sehemu husika kabla mzozo kuanza, mtu wa kwanza kupokea simu. Nitakwenda sehemu za vita. Nitazungumza na pande zote. Nitafanya kazi kwa kushirikiana na Baraza la Usalama, na mataifa wanachama, na nitakuwa mpatanishi miongoni mwa wapatanishi,” Grynspan alisema.
Tangu kuanzishwa kwa Shirika hilo 1945 hakujakuwa na Katibu Mkuu mwanamke, ingawa wamekuwa manaibu Katibu Wakuu wanawake kadhaa ikiwemo Asha-Rose Migiro wa Tanzania na Amina Mohammed wa Nigeria.
Katibu Mkuu wa 10 wa Umoja wa Mataifa anatarajiwa kuanza majukumu yake Januari 1, 2027.
Wakati mchakato ukiendelea, je, kuna matumaini ya mwanamke mmoja kuibuka kidedea kati ya wagombea hao wawili?














