| Swahili
ULIMWENGU
2 dk kusoma
Shirikisho la Utalii Kenya lapinga wito wa Gachagua kwa watalii kutoitembelea nchi hiyo
Aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua, ametoa wito kwa watalii na wawekezaji kutozuru Kenya hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027, kwa madai ya ukosefu wa usalama.
Shirikisho la Utalii Kenya lapinga wito wa Gachagua kwa watalii kutoitembelea nchi hiyo
KTF ilionya kuwa kauli za aina hiyo zinaweza kuathiri imani ya wageni kuhusu Kenya kama eneo salama la utalii na kuharibu shughuli za kiuchumi. / / Reuters

Shirikisho la Utalii la Kenya (KTF) limepinga kauli za aliyekuwa Naibu Rais wa Kenya, Rigathi Gachagua, aliyetoa wito kwa watalii na wawekezaji kutozuru Kenya hadi baada ya Uchaguzi Mkuu wa mwaka 2027.

Kauli hiyo ya KTF imekuja baada ya Gachagua, akizungumza wakati wa ibada ya Jumapili huko Kirinyaga, kudai kuwa hali ya sintofahamu ya kisiasa nchini Kenya imeifanya nchi hiyo kuwa si salama kwa utalii na uwekezaji wa kigeni. Alisema wageni wanapaswa kusubiri hadi hali ya utulivu irejee.

"Tunakabiliwa na hali ya machafuko, hali ambayo watu wanaweza kuamua kuchukua silaha dhidi ya serikali na dhidi ya wahuni wanaotumiwa na serikali," alisema, akiashiria ongezeko la madai ya ghasia za kisiasa zinazodaiwa kufadhiliwa.

"Hatuna tena usalama hata kwa watalii katika nchi hii. Kuna wahuni wengi kila mahali, na ningewataka watalii kusitisha ziara zao nchini Kenya hadi mwaka ujao. Tukabiliane na utawala huu, tuondoe wahuni na polisi wanaokiuka sheria, kisha mnaweza kuja," alisema.

Katika taarifa yake ya Jumatatu, KTF ilisema watalii wanaoitembelea Kenya hawahusiki na siasa za ndani na hawalengwi na makundi yanayohusika katika mivutano ya kisiasa.

"Wanakuja kufurahia wanyamapori wa Kenya, fukwe, utamaduni, ukarimu wa wananchi, mikutano, pamoja na matukio ya michezo. Hawahusiki wala hawalengwi na ushindani wa kisiasa ambao wakati mwingine hujitokeza nchini mwetu," ilisema sehemu ya taarifa hiyo.

KTF ilionya kuwa kauli za aina hiyo zinaweza kuathiri imani ya wageni kuhusu Kenya kama eneo salama la utalii na kuharibu sekta inayosaidia mnyororo mkubwa wa shughuli za kiuchumi.

"Imani ikishaharibiwa, kuijenga tena kunaweza kuchukua miaka, na wakati mwingine hata zaidi, bila kujali kasi ya mabadiliko ya hali ya kisiasa," ilisema KTF.

Shirika hilo lilieleza kuwa wafanyakazi wa hoteli, waongoza watalii, madereva, mafundi wa bidhaa za sanaa, wakulima, wasanii, waendeshaji biashara za ufukweni, mashirika ya ndege, mawakala wa safari na maelfu ya wafanyabiashara wadogo hutegemea mtiririko wa wageni ili kujipatia kipato.

KTF imewataka wanasiasa kutoitumia sekta ya utalii na sekta nyingine muhimu kama sehemu ya mapambano yao ya kisiasa, huku wakitatua tofauti zao bila kuwaweka Wakenya wengi katika hatari.