Bunge la Ufaransa limepiga kura kwa pamoja kuondoa amri ya karne kadhaa za kifalme ambazo ziliorodhesha utumwa wakati wa ukoloni, kuashiria hatua muhimu kwa nchi hiyo kutafakari kuhusu enzi zake za ukoloni.
Wabunge waliidhinisha sheria iliyofuta “Code Noir,” sheria kadhaa za karne ya 17 na 18 ambazo ziliratibu utumwa kote katika makoloni ya Ufaransa. Sheria hiyo iliidhinishwa kwa kura 254-0, kulingana na matokeo ya bunge.
Pamoja na kuwa utumwa ulifutwa Ufaransa 1848, amri hizo hazikubatilishwa rasmi.
Sheria hiyo bado inahitaji kuidhinishwa na Bunge la Seneti kabla kutumika rasmi. Kura ya Seneti bado haijaratibiwa.
Rais wa Ufaransa Emmanuel Macron aliunga mkono kufutwa kwa sheria hiyo mapema mwezi huu, akisema kuwa kuendelea kuwepo kwa amri hizo kulikuwa kunaenda kinyume na maadili ya taifa la Ufaransa.
Sheria ya Utumwa
Akizungumza katika Ikulu ya Elysee wakati wa kuadhimisha miaka 25 tangu Ufaransa ilipotambua utumwa na biashara ya utumwa kuwa uhalifu dhidi ya binadamu, Macron amesema Ufaransa inatakiwa kukabiliana na historia yake kwa uwazi na kukiri kuwa mateso yaliyosababishwa na utumwa hayawezi kurekebishwa.
Yael Braun-Pivet, rais wa Bunge, alieleza kuridhishwa na kura hiyo kupitia mtandao wa kijamii wa Marekani wa X akitaja uamuzi huo “kwa jina la ubinadamu, usawa, na kilimwengu.”
Aliongeza kuwa Ufaransa lazima “ieleze bila kufuta, kukiri kuhusika,” wakati nchi hiyo ikiendelea kukabiliana na historia yake “kwa uwazi” miaka 25 baada ya sheria ya Taubira kutambua utumwa kama uhalifu dhidi ya binadamu.
Mjadala huu kuhusu “Sheria ya Utumwa” unakuja huku kukiwa na wito kutoka kwa wanaharakati na wabunge kwa Ufaransa kushughulikia suala la utumwa, ukoloni na ubaguzi wa rangi.


















