| Swahili
MICHEZO
2 dk kusoma
Bondia wa zamani bingwa wa dunia Zolani Tete auawa kwa kupigwa risasi nchini Afrika Kusini
Maafisa walisema kuwa Zolani Tete alikuwa akiwasili nyumbani kwake katika eneo la Mdantsane wakati wanaume wawili wenye silaha, waliokuwa wamevalia barakoa zinazofunika uso mzima, waliposhuka kutoka kwenye gari na kufyatua risasi.
Bondia wa zamani bingwa wa dunia Zolani Tete auawa kwa kupigwa risasi nchini Afrika Kusini
Zolani Tete akisherehekea baada ya kumshinda Jason Cunningham katika pambano lao la uzani wa 'super-bantamweight' mnamo Julai 2022. / reuters

Bingwa wa zamani wa dunia wa ngumi, Zolani "Last Born" Tete, alipigwa risasi na kufariki dunia nje ya nyumba yake katika jimbo la Eastern Cape nchini Afrika Kusini siku ya Ijumaa, kwa mujibu wa polisi na waziri wa michezo wa nchi hiyo.

Mwanamichezo huyo mwenye umri wa miaka 38 alikuwa akiwasili nyumbani kwake katika eneo la Mdantsane wakati wanaume wawili wenye silaha, waliokuwa wamefunika nyuso zao kwa barakoa, waliposhuka kutoka kwenye gari na kuanza kufyatua risasi.

"Sitatoa nadharia yoyote kuhusu nani aliyefanya hivi au sababu yake," Waziri wa Michezo Gayton McKenzie alisema katika taarifa.

Mauaji ya Tete yataibua upya mjadala kuhusu uhalifu wa kutumia nguvu nchini Afrika Kusini, nchi ambayo inaendelea kuwa na mojawapo ya viwango vya juu zaidi vya mauaji duniani licha ya kupungua kwa matukio hayo hivi karibuni.

Mauaji ya bingwa huyo wa dunia pia yameleta simanzi kubwa huko Mdantsane, eneo ambalo limetoa baadhi ya mabondia waliofanikiwa zaidi nchini Afrika Kusini.

Sababu haijajulikana

Mwanamke mwenye umri wa miaka 27 aliyekuwa akisafiri na Tete alipigwa risasi kadhaa na kukimbizwa hospitalini. Polisi wameanzisha uchunguzi na sababu ya shambulio hilo bado haijajulikana.

Tete alishinda taji la dunia la IBF katika uzani wa 'junior-bantamweight' mwaka 2014 baada ya kumshinda Mjapani Teiru Kinoshita jijini Kobe. Baadaye alishinda taji la WBO katika uzani wa 'bantamweight'.

Anakumbukwa zaidi kimataifa kwa ushindi wake wa 'knockout' wa sekunde 11 dhidi ya bondia mwenzake wa Afrika Kusini, Siboniso Gonya, jijini Belfast mnamo Novemba 2017—ushindi wa haraka zaidi kuwahi kushuhudiwa katika pambano la kuwania taji la dunia.


CHANZO:reuters