| Swahili
UTURUKI
2 dk kusoma
Uturuki itaendelea na mapambano dhidi ya kundi la kigaidi la FETO: Erdogan
Rais wa Uturuki, Recep Tayyip Erdogan, amesema kuwa makundi ya kigaidi yameishiwa na mbinu hayana tena nafasi ya kufanikiwa katika juhudi zao dhidi ya nchi hiyo.
Uturuki itaendelea na mapambano dhidi ya kundi la kigaidi la FETO: Erdogan
Erdogan ametoa hotuba katika hafla ya kuadhimisha miaka 10 tangu jaribio la mapinduzi lililofeli la Julai 15 jijini Ankara. / / AA

Uturuki itaendelea na mapambano yake dhidi ya Shirika la Kigaidi la Fetullah (FETO) kwa kuzingatia sheria hadi pale tishio hilo litakapokomeshwa kabisa, Rais Recep Tayyip Erdogan alisema Jumatano, wakati wa maadhimisho ya miaka 10 tangu jaribio la mapinduzi lililoshindwa la Julai 15, 2016.

Akizungumza katika hafla ya kumbukumbu iliyofanyika Ankara yenye kaulimbiu "Miaka 10 ya Julai 15: Uamuzi ni Wetu, Ushindi ni Wetu," Erdogan aliwakumbuka mashahidi 253 waliouawa na maelfu waliojeruhiwa wakati wa jaribio hilo la mapinduzi, huku akiwapongeza wote waliopinga waasi hao.

"FETO bado ipo, na kwa hiyo mapambano dhidi ya FETO yataendelea," alisema Erdogan. "Tutaendelea na mapambano yetu dhidi ya FETO kwa uvumilivu na kwa kuzingatia sheria hadi hatari hiyo itakapokomeshwa kabisa."

Alisema mamlaka zitaendelea kuwafuatilia wanaodaiwa kuwa wanachama wa siri wa kundi hilo, huku zikiepuka "mitego ambayo FETO inataka kututega" na kuchukua tahadhari katika kila hatua.

"Kila mtu sasa anapaswa kuelewa kwamba mashirika ya kigaidi yameshiwa na mbinu. Hakuna mafanikio yanayoweza kupatikana kupitia uadui dhidi ya Uturuki," alisema Erdogan.

Erdogan aliishutumu FETO, ambayo Uturuki inaamini ndiyo ilipanga jaribio la mapinduzi la mwaka 2016, kwa kushambulia taasisi muhimu za serikali, zikiwemo Bunge, Ikulu ya Rais, Makao Makuu ya Jeshi, vituo vya polisi, shirika la habari la TRT, na kampuni ya mawasiliano ya satelaiti ya Turksat wakati wa jaribio hilo la kutwaa madaraka.

Alisema sifa kuu ya shirika hilo ni kuwa "mtandao wa ujasusi unaoula mwili kutoka ndani kama seli za saratani," akisisitiza kuwa Uturuki itaendelea kulipiga vita hadi litakapokomeshwa kabisa.

"Moyo wa kupigania uhuru ulifufuka"

Rais huyo pia aliwapongeza wanajeshi, polisi na raia waliokabiliana na jaribio la mapinduzi, akisema walilinda demokrasia na matakwa ya wananchi.

"Usiku huo tuliona moyo wa kupigania Uhuru ukifufuka tena," alisema Erdogan, akiongeza kuwa wananchi wa Uturuki walionyesha kwamba "hakuna nguvu inayoweza kusimama mbele ya taifa hili."

Jaribio hilo la mapinduzi lililoshindwa lilisababisha vifo vya mashahidi 253, huku watu 2,734 wakijeruhiwa, lilipangwa na kutekelezwa na Shirika la Kigaidi la Fetullah (FETO).

Erdogan pia aliahidi kuwa Uturuki itaendelea kuwaunga mkono "watu wanaodhulumiwa na wanaoteseka kuanzia Gaza hadi Lebanon, Somalia hadi Syria, na kutoka Rakhine hadi Sudan."

"Popote palipo na mtu anayedhulumiwa au mwathirika anayelia kwa huzuni, tutaendelea kusimama pamoja nao," alisema, akiongeza kuwa wale wanaojaribu kudhoofisha nafasi ya Uturuki hawatafanikiwa.

CHANZO:AA