Kiwanda cha Dangote cha kusafisha mafuta nchini Nigeria kimeanza kuuza mafuta kwa Dola za Marekani katika soko la ndani, ikieleza kuwa imefikia uamuzi huo kutokana na ugumu wa kupata mafuta ghafi ya kutosha kupitia mpango wa serikali wa kununua mafuta ghafi kutumia sarafu ya Naira, pamoja na kupanda kwa bei ya mafuta katika soko la kimataifa.
Akizungumza siku ya Jumanne, msemaji wa kampuni alisema kuwa upungufu wa mafuta ghafi yanayotolewa chini ya mpango huo umeifanya kampuni ishindwe kuendelea kuuza mafuta kwa sarafu ya Nigeria, Naira, wakati inanunua malighafi kwa Dola za Marekani.
Mpango wa kununua mafuta ghafi kutumia sarafu ya Naira, ulioanzishwa Oktoba 2024, ulilenga kuwaruhusu wasafishaji wa mafuta nchini kununua mafuta ghafi kwa kutumia sarafu ya Nigeria, naira, ili kupunguza matumizi ya fedha za kigeni na kuimarisha soko la ubadilishaji wa fedha.
Kiwanda cha Dangote, ambacho ni kikubwa zaidi barani Afrika na kina uwezo wa kusafisha mapipa 700,000 ya mafuta ghafi kwa siku, kimeweka bei mpya za bidhaa zake ambapo petroli itauzwa kwa Dola 0.779 kwa lita, dizeli kwa dola 1.087 kwa lita, na mafuta ya ndege kwa Dola 0.942 kwa lita. Bei hizo zimo kwenye jedwali la bei lililotolewa kwa wasambazaji wa mafuta.
Makamu wa Rais wa Dangote Group, Edwin Devakumar, alisema kampuni imekuwa ikibeba mzigo wa tofauti ya thamani ya sarafu kwa kuuza mafuta kwa Naira huku ikinunua mafuta ghafi kwa Dola za Marekani. Hata hivyo, alisema upatikanaji mdogo wa mafuta ghafi kupitia mpango wa kununua mafuta ghafi kutumia Naira umeufanya mfumo huo ushindwe kuendelea kufanya kazi kwa ufanisi.
Mahitaji ya Dola yanatarajiwa kuongezeka
Ingawa Kampuni ya Taifa ya Mafuta ya Nigeria (NNPC) iliongeza kiwango cha mafuta ghafi kinachopelekwa Dangote hadi shehena saba mwezi Mei kutoka wastani wa shehena tano hapo awali, kampuni hiyo imesema inahitaji kati ya shehena 13 na 15 kila mwezi ili kuendesha shughuli zake kikamilifu.
Uamuzi huo unaweza kuongeza mahitaji ya dola miongoni mwa wauzaji wa mafuta na kufanya bei za mafuta za ndani kuwa nyeti zaidi kwa mabadiliko ya viwango vya ubadilishaji wa fedha.
Kutokana na upungufu huo, imelazimika kuagiza mafuta ghafi yaliyobaki kutoka soko la kimataifa kwa bei za kimataifa.













