Changamoto za mafuriko nchini Msumbiji
AFRIKA
2 dk kusoma
Changamoto za mafuriko nchini MsumbijiMafuriko yamesababisha watu karibu 392,000 nchini Msumbiji kuondoka katika makazi yao tangu mwanzoni mwa mwaka huu, kudhihirisha namna mabadiliko ya tabianchi yanavyotonesha kidonda cha migogoro na kulazimisha familia kuanza maisha yao upya.
Mafuriko nchini Msumbiji yameathiri maeneo ambayo tayari yalikuwa yameharibiwa na vimbunga na ukame . / Reuters
9 Februari 2026

Wakati mto ulipovunja kingo zake katika Mkoa wa Gaza nchini Msumbiji, Celina Guaza alichukua mfuko wake ambao aliukuwa ameuandaa tayari, kumueleka mgongoni mjukuu wake na kuondoka.

Nyumba yao ilizama kwenye maji hayo. Picha zao za kumbukumbu pamoja na vyeti vya kuzaliwa zilisombwa na maji.

Hii siyo mara ya kwanza kwa wao kuondolewa katika makazi yao. Mwaka 2000, Celina alipoteza nyumba yake kutokana na mafuriko. Miaka 13 baadaye, mkosi ukawakabili tena na kuharibu mimea yao yote. Sasa, 2026, mafuriko tena yamewaharibia makazi yao.

"Upepo mkali unavuma, viwango vya maji vikapanda, na inabidi tuanze tena upya," Celina ameiambia TRT Afrika.

Tangu mwanzoni mwa mwaka, mafuriko mabaya yametokea katika maeneo ya kusini na katikati mwa Msumbiji, na kufanya watu karibu 392,000 kupoteza makazi yao.

Hatari zaidi

Mafuriko ya hivi karibuni yamekuja kwa kasi zaidi.

"Watoto walikuwa wanalia, watu wazima walikuwa wanashindwa kutembea, lakini hakukuwa na muda hata wa kufikiria. Tulikimbia kuokoa maisha yetu. Katika hali hiyo ya taharuki, sikumuona mpwa wangu kwa siku mbili," anakumbuka João Nhabanga kutoka Mkoa wa Maputo. "Tulimpata katika sehemu moja ya maduka, akiwa anatetemeka. Lakini sijui watu wangapi ambao hawakuwa na bahati?"

Hatua za kuzuia na mikakati ya serikali, pamoja na misaada kutoka washirika na sekta binafsi, kumesaidia kuepuka mkasa mkubwa. Karibu watu 20,000 waliokolewa kwa njia ya angan, maji na barabara.

Watu karibu 100,000 sasa wanaishi katika maeneo karibu 100 ya muda – zaidi katika shule na majengo ya serikali – wakisubiri ujenzi mpya.

Watu kuwa wengi katika sehemu hizi kunasababisha hatari. Huduma muhimu hazipatikani. Katika maeneo yaliyojaa watu, wanawake na wasichana wanakabiliwa na tatizo lingine la unyanyasaji wa kijinsia na udhalilishaji.

Vitisho vinavyoendelea

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulikia Wakimbizi, UNHCR limepeleka maafisa wake katika maeneo ya Mkoa wa Gaza kuwatambua wale walio kwenye hatari zaidi. Juhudi za shirika hilo zinaangazia kuimarisha kuepuka na mifumo ya kushughulikia matatizo, ikiwemo msaada wa kisaikolojia.

Lakini viwango vya hatari vinafanya juhudi hizi kutoweza kufikia malengo. Mashirika ya misaada yanasema Msumbiji inahitaji misaada kutoka kwa jamii ya kimataifa kuimarisha shughuli zao kwa watu.

Kuendelea kwa mafuriko katika nchi hiyo ya kusini mwa Afrika ni ishara ya hali kuwa mbaya zaidi kutokana na mabadiliko ya tabianchi na mgogoro. Na huku kukiwa na misitu ya mvua, hatari ya uharibifu mwingine bado ipo.

CHANZO:TRT Afrika