Neymar ametangaza kustaafu soka la kimataifa baada ya Brazil kufungwa mabao 2-1 na Norway katika hatua ya 16 bora ya Kombe la Dunia la FIFA, matokeo yaliyowaondoa mabingwa hao mara tano kwenye mashindano hayo.
"Nilijaribu. Nilijaribu. Ilianzia hapa kwenye Uwanja wa MetLife na nimehitimishia hapa. Sasa imekwisha," Neymar aliwaambia waandishi wa habari baada ya mechi hiyo ya Jumapili.
Alianguka chini huku akitokwa na machozi baada ya filimbi ya mwisho kupulizwa uwanjani hapo New Jersey, kabla ya kufarijiwa na wachezaji wenzake.
Mchezaji huyo mwenye umri wa miaka 34 alifunga bao pekee la Brazil kwa mkwaju wa penalti katika dakika ya 10 ya muda wa nyongeza, lakini hilo halikutosha kuzuia kuondolewa kwao, huku Norway ikitinga robo fainali ya Kombe la Dunia kwa mara ya kwanza.
Neymar anastaafu akiwa ndiye mfungaji bora wa muda wote wa Brazil, akiwa na mabao 80 ya kimataifa katika mechi 130 alizoichezea timu hiyo. Alianza kuichezea timu ya taifa ya wakubwa mwaka 2010 baada ya kuanza taaluma yake ya soka la kulipwa katika klabu ya Santos FC mwaka 2009, na alishinda medali ya dhahabu ya Olimpiki akiwa na Brazil mwaka 2016.
Mwisho wa enzi
Neymar alicheza mechi yake ya kwanza kuwakilisha Brazil mnamo Agosti 9, 2010 — mechi ya kirafiki dhidi ya Marekani iliyofanyika katika uwanja wa Meadowlands, kaskazini mwa New Jersey.
Kutokana na jeraha la muda mrefu kwenye msuli wa mguu wake wa kulia, Neymar alicheza mechi mbili pekee kati ya tano ambazo Brazil ilishiriki katika mashindano hayo. Pia alicheza kwa dakika 15 dhidi ya Scotland katika hatua ya makundi.
Mchezaji bora wa Brazil kwa zaidi ya muongo mmoja alikuwa akikabiliwa na changamoto ya majeraha katika miaka ya hivi karibuni, jambo lililopunguza mchango wake uwanjani. Sasa nchi hiyo inaingia katika kipindi cha mpito, huku kizazi kipya kikichukua nafasi hiyo.
"Tunaomba watu wawe na subira kwa kizazi hiki kipya na kuwaunga mkono tangu mwanzo," alisema nahodha Marquinhos.











