Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) na Uganda zimeingia makubaliano sita ambayo yanalenga kukuza ushirikiano kati ya nchi hizo mbili.
Makubaliano hayo yatasainiwa mbele ya viongozi wa mataifa hayo, Félix Tshisekedi na Yoweri Museveni, siku ya Jumatatu.
Haya yanajiri baada ya kikao cha pamoja kati ya nchi hizo, kilichofanyika kuanzia Mei 8 hadi 10 jijini Kampala.
Moja ya mambo yatakayoangaziwa katika makubaliano hayo ni pamoja na ushirikiano wa ulinzi wa mipaka na uhusiano wa kibiashara.
Maeneo mengine ni pamoja na sekta ya habari, biashara, teknolojia, utalii, uvuvi na kilimo.
Wakati wa mkutano wao, mawaziri kutoka nchi hizo walikubaliana kuimarisha uhusiano kati ya nchi hizo jirani.
Wakati huo huo, nchi hizo zinalenga kujenga kituo cha pamoja cha forodha na masoko ya kisasa ya mipakani katika maeneo ya Kasindi, Bunagana na Mahagi.
















