Wenyeji Morocco watachuana na mabingwa watetezi Afrika Kusini usiku wa leo katika mojawapo ya mechi kubwa za robo fainali ya Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON).
Mechi hiyo itakayochezwa katika Uwanja wa Moulay El Hassan jijini Rabat ni marudio ya fainali waliocheza WAFCON ya mwaka 2022, ambapo Afrika Kusini iliifunga Morocco mabao 2–1 na kutwaa taji lao la kwanza la bara.
Miaka minne baadaye, dau la mchezo huo ni kubwa zaidi.
Kwa upande wa Morocco, faida ya kucheza nyumbani itakuwa muhimu sana. Timu ya 'Atlas Lionesses' ina fursa ya kufika nusu fainali mbele ya mashabiki wao na kuendeleza harakati za kutafuta taji lao la kwanza la WAFCON. Pia wanajua kuwa kufika hatua ya nne bora kutawahakikishia nafasi ya kushiriki Kombe la Dunia la Wanawake la FIFA la mwaka 2027 nchini Brazil.
Afrika Kusini inakuja na uzoefu wa kuwa mabingwa watetezi, lakini safari yao kuelekea robo fainali haikuwa rahisi. Walianza kampeni yao kwa kufungwa mabao 2–1 na Tanzania kabla ya kujikwamua na kufanikiwa kusonga mbele kutoka hatua ya makundi.
Deni la soka na kisasi
Hata hivyo, uzoefu wao katika mashindano haya unamaanisha kuwa wanaifahamu vyema presha inayokuja na mechi za mtoano.
Pia kuna deni la soka kati ya timu hizi mbili. Morocco itakuwa ikitafuta kulipa kisasi cha kufungwa katika fainali ya mwaka 2022, huku Afrika Kusini ikitaka kuonyesha kuwa bado ndiyo timu tishio na inayopaswa kushindwa katika soka la wanawake barani Afrika.
Mechi itaanza saa tatu usiku kwa saa za huko Rabat. Mshindi atasonga mbele hadi nusu-fainali na kujihakikishia nafasi ya moja kwa moja katika Kombe la Dunia la Wanawake la mwaka ujao.
Kwa kuzingatia umuhimu mkubwa wa mechi hii, sio mchezo wa kawaida tu wa robo-fainali; ni marudio ya mojawapo ya fainali muhimu zaidi katika soka la wanawake barani Afrika, huku nafasi ya kushiriki Kombe la Dunia ikiwa hatarini.














