Uturuki imeomba Interpol kutoa 'notisi nyekundu' dhidi ya Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu, ikiwa ni sehemu ya kesi inayoendelea kuhusiana na shambulio dhidi ya wanaharakati waliokuwa kwenye msafara wa meli wa Global Sumud Flotilla, ambao ulikuwa ukisafirisha misaada ya kibinadamu kwenda Gaza; haya yamesemwa na Waziri wa Sheria Akin Gurlek.
Katika taarifa iliyowekwa kwenye mtandao wa kijamii wa Uturuki wa NSosyal siku ya Ijumaa, Gurlek alisema kuwa kesi inaendelea katika Mahakama ya 11 ya Jinai ya Ngazi ya Juu ya Istanbul dhidi ya washitakiwa 35, akiwemo Netanyahu na Afek Moskovitch, kuhusiana na tukio hilo lililotokea katika maji ya kimataifa.
Alisema kuwa hati za kukamatwa kwa Netanyahu na Moskovitch zilizotolewa tarehe 14 Julai 2026, kwa tuhuma za "mauaji ya halaiki," ziliifanya Wizara ya Sheria kuiomba Wizara ya Mambo ya Ndani kutafuta notisi nyekundu za Interpol kwa washukiwa hao wawili.
Nyaraka husika pia zimekabidhiwa kwa Wizara ya Mambo ya Nje, alisema Gurlek.
Alisema Netanyahu na Moskovitch wanashitakiwa kwa vitendo vinavyodaiwa kuhusisha "uingiliaji kati wa kijeshi dhidi ya raia waliokuwa wakipeleka misaada ya kibinadamu Gaza katika maji ya kimataifa na kuwekwa kizuizini kwa wanaharakati."
Tuhuma hizo zinajumuisha "uhalifu dhidi ya binadamu," "mauaji ya halaiki," "kunyimwa uhuru kwa njia nzito," "kusababisha majeraha kwa makusudi," "utesaji," "uharibifu wa mali," "wizi wa kutumia nguvu uliokithiri" na "kuteka nyara chombo cha usafiri," aliongeza.
"Hatutaruhusu uhalifu uliofanywa Gaza kufichwa au wahusika kulindwa na kinga dhidi ya kuwajibishwa," alisema Gurlek.
"Tutatumia kwa uthabiti njia zote zinazopatikana chini ya sheria za kitaifa na kimataifa," aliongeza.
Mnamo Novemba 2025, Uturuki ilitoa hati za kukamatwa kwa Netanyahu na washukiwa wengine kadhaa kutokana na kuhusika kwao katika mauaji ya halaiki huko Gaza.
Hati hizo zilitolewa baada ya uchunguzi wa kina kuhusu mashambulio ya "kimfumo" ya Israel dhidi ya raia huko Gaza, vitendo vya mauaji ya halaiki na uhalifu dhidi ya binadamu.
UTURUKI
2 dk kusoma
Uturuki yataka ilani nyekundu ya Interpol dhidi ya Netanyahu kufuatia shambulio dhidi ya fotilla
Ankara inasema haitaruhusu uhalifu uliofanywa Gaza kufichwa au wahusika kulindwa dhidi ya kuwajibishwa.

Soma zaidi



















