Uturuki imewakumbuka walioathirika katika mashambulizi ya ubaguzi wa rangi 1993 mji wa Ujerumani wa Solingen ambapo watu watano kutoka familia moja ya Kituruki waliuawa, huku ikisisitiza dhamira yake ya kukabiliana na ubaguzi wa rangi, chuki, na chuki dhidi ya Uislamu.
Siku ya Ijumaa, katika kumbukumbu ya watu wa familia ya Genc waliouawa kwenye shambulizi hilo, Wizara ya Mambo ya Nje ya Uturuki ilisema: “Katika hafla hii, kwa mara nyingine tunamuenzi Mevlude Genc kwa heshima na taadhima.”
Genc, ambaye alifariki 2022 akiwa na umri wa miaka 80, alikuwa ishara ya maridhiano Ujerumani baada ya kupoteza mabinti wawili, wajukuu wawili, na mpwa wake katika mkasa wa moto wa 1993 wa wafuasi wa siasa za mrengo wa kulia mjini Solingen.
Msimamo wa kupigiwa mfano
Wizara hiyo ilipongeza msimamo wake wa kupigiwa mfano na wito wa utulivu licha ya kupoteza watu wa familia yake kwenye shambulizi hilo.
Kwa kusisitiza msimamo wa Uturuki dhidi ya ubaguzi, wizara imesema Uturuki itaendelea na makabiliano dhidi "ya kuongezeka kwa ubaguzi wa rangi, chuki kwa raia wa kigeni na chuki dhidi ya Uislamu katika majukwaa yote."
Mei 29, 1993, vijana wanne wa kiume kati ya umri wa miaka 16 na 23 walichoma moto nyumba ya familia ya Genc, na kuwaua watu watano pamoja na kuwajeruhi wengine 14.
Watatu kati ya walioshambulia walihukumiwa kifungo cha miaka 10 gerezani huku mmoja akifungwa miaka 15 jela.



















