Rais Donald Trump ameapa kuwa Marekani haitasahau kamwe mashambulizi ya Septemba 11, 2001, na kudokeza kwamba nchi hiyo inaendelea na “vita dhidi ya ugaidi” miaka 25 baadaye kwa kuishambulia Iran.
Akizungumza katika jengo la Wizara ya Ulinzi la Pentagon siku ya Ijumaa, baada ya kutohudhuria hafla kuu ya kukumbuka 9/11 iliofanyika New York, Trump pia aliwashambulia “wenye msimamo mkali” wa ndani ya Marekani, katika kauli iliyoonekana kuwalenga wanachama wa Chama cha Democratic.
“Leo tunakula upya kiapo kitakatifu tulichokula kwa mara ya kwanza kwa heshima yao miaka 25 iliyopita. Hatutasahau kamwe, kamwe. Ndiyo maana tunapigana leo,” Trump alisema.
“Hatutakuwa na chaguo. Kinachoweza kuwepo ni ushindi pekee. Tunapigana kwa nguvu. Tunapigana ili kushinda,” aliongeza rais huyo.
Moja ya ndege zilizotekwa nyara katika mashambulizi ya 9/11 iliigonga jengo la Pentagon jijini Washington, na kuua watu 184, ambao walikumbukwa katika hafla hiyo.
Hata hivyo, marais waliotangulia wamekuwa wakitumia siku hiyo muhimu ya mashambulizi hayo kutembelea maeneo kadhaa, yakiwemo New York, ambako idadi kubwa ya waathiriwa 2,977 waliuawa katika mashambulizi dhidi ya majengo ya World Trade Center.
Trump aliendelea kuhusisha kile kinachoitwa “vita dhidi ya ugaidi” vilivyoanzishwa na mtangulizi wake wa chama cha Republican, George W. Bush, na vita vya Marekani na Israel dhidi ya Iran, ambavyo sasa vimeingia mwezi wa saba.
“Leo tunawatambua wanajeshi wote wa Marekani waliohudumu katika ‘Vita dhidi ya Ugaidi.’ Hivi ni vita dhidi ya ugaidi na vya kutisha sana,” Trump alisema.
“Na tunawatambua wanajeshi wanaofanya kazi hivi sasa kuhakikisha kwamba Iran, ambayo ni mfadhili mkuu wa ugaidi duniani, haitawahi kuwa na silaha ya nyuklia.”
Vita vya Iran vyaendelea
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, pia aliishambulia Iran kwa maneno katika hotuba yake wakati wa hafla hiyo iliyofanyika Pentagon.
“Katika kipindi cha miezi sita iliyopita, tumeangamiza kwa kiwango kikubwa nchi ambayo ni mfadhili mkuu wa ugaidi duniani. Wapiganaji wetu wamekabiliana na utawala unaoendeshwa kwa mfumo wa Kiislamu ambao umetaka kuona vifo vyetu kwa karibu nusu karne,” Hegseth alisema.
Vita vya Iran vyaendelea, huku Iran ikiendelea kwa kiasi kikubwa kudhibiti Mlango-Bahari wa Hormuz, licha ya kuendelea kushamabuliana na Marekani mara kwa mara.
Trump pia alielekeza kauli zake kwenye siasa za ndani, siku moja baada ya mkutano wa chama cha Republican kuhusu uchaguzi wa nusu muhula nchini Marekani. Katika mkutano huo, Trump na Makamu wa Rais JD Vance waliwashutumu Democrats kwa kuonyesha huruma kwa washambuliaji wa 9/11.
"Kizazi kimoja baada ya tukio la 9/11, tunajua pia kwamba jibu la mwisho kwa ukatili huo na ushindi wa kweli dhidi ya wahusika hautapatikana katika uwanja wa vita wa nchi za kigeni," alisema Trump.
Akisimulia kisa cha zima-moto aliyeuawa katika mashambulizi hayo, ambaye mwanawe baadaye alikuja kuwa mkongwe wa Jeshi la Wanamaji la Marekani, Trump alisema kuwa hilo lilionyesha kuwa "tunaweza kuwa taifa ambalo mashujaa wake si watu wenye msimamo mkali kwa ajili ya sababu isiyo dhahiri."


















