Idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko Kenya yafikia 62
Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Kenya inaonya kuendelea kuwepo kwa mafuriko na hatari ya dhoruba katika sehemu za mwanzo za msimu huu wa mvua ndefu.
Mamlaka ya Hali ya Hewa nchini Kenya imeonya kuwa nchi inapaswa kutarajia mvua kubwa zitakazoendelea kunyesha katika maeneo tofauti ya nchi.
Idadi ya waliofariki kutokana na mafuriko katika baadhi ya maeneo ya nchi kufikia Machi 6 ni 62, Kitengo cha Kitaifa cha Kukabiliana na Maafa nchini Kenya kimethibitisha.
Hii inajumuisha wanaume 46, wanawake 8 na watoto 8.
Mji mkuu wa Kenya Nairobi ndio wenye idadi kubwa zaidi ya vifo 33.
Huku eneo la Mashariki linafuatia kwa vifo 17, na eneo la Bonde la Ufa likiwa na 7.
Kwengineko, mikoa ya Nyanza na Pwani kila moja imerekodi vifo 2 na Kanda ya Kati kifo kimoja.
Mikoa kadhaa ya nchi inaendelea kukumbwa na mvua kubwa.
Wataalamu wa hali ya hewa wanaonya kuhusu mafuriko ya ghafla na hatari za dhoruba katika sehemu za mwanzo za msimu huu wa mvua ndefu zinazoendelea.
Wanasema hata hivyo kiwango cha mvua kinaweza kubadilika kwa mwezi.
Machi 13, 2026, Kenya ilichukua hatua kubwa kuimarisha mifumo yake ya kutabiri hali ya hewa baada ya Rais William Ruto kuidhinisha Mswada wa Hali ya Hewa wa Kenya, 2023. Hii ni kwa ajili ya kuandaa njia ya kuundwa kwa Mamlaka ya Huduma ya Hali ya Hewa ya Kenya.
Hii inatarajiwa kupanua mamlaka ya idara ya kudhibiti, kuratibu na kutoa huduma zinazohusiana na hali ya hewa kwa haraka kote nchini.