Rais wa Shirikisho la Soka barani Ulaya (UEFA) Aleksander Ceferin anasema hana nia ya kugombea nafasi ya Rais wa FIFA Gianni Infantino lakini anaonya kuwa Infantino atakabiliwa na upinzani iwapo atataka kugombea tena kwenye uchaguzi wa mwezi Machi.
Infantino amekabiliwa na shinikizo baada ya kuachana na mpango wake wa kuuza hisa za Kombe la Dunia kwa wawekezaji binafsi. UEFA na mashirikisho mengine walipinga mapendekezo hayo, huku UEFA ikitishia kususia mashindano ya FIFA.
Ceferin alishtumu mpango huo katika mahojiano ya kipindi cha podcast ‘The Rest is Politics’, akiutaja kuwa “mbovu kuliko mpango wa Super League.”
“Nina uhakika kuwa mpango huo [FFE] haupo tena. Kwangu mimi, jambo muhimu ni kwamba tumezuia jaribio lingine la kutaka kuweka rehani mchezo.” alisema.
Ceferin alisema Infantino sasa anaweza kuchagua kati ya mawili: aondoke madarakani baada ya kupoteza kuungwa mkono na wadau wa soka au agombee kwenye uchaguzi na kukabiliana na mpinzani.
“Moja ni atambue kuwa haungwi tena mkono, na siyo tu kutoungwa mkono na wale wanaopiga kura pekee, lakini kutoungwa mkono kabisa na wadau wa soka, mashabiki, wachezaji, wachezaji wa zamani, makocha.
“Ya pili ni kuwa ashiriki uchaguzi mwezi Machi, lakini kwa hali hiyo, nadhani kutakuwa na mgombea dhidi yake. Sijajua atakuwa nani.”
Infantino ameiongoza FIFA tangu 2016 na ameonekana kama atashinda bila kupingwa katika uchaguzi wa mwaka ujao nchini Morocco. FIFA imeweka Novemba 18 kama siku ya mwisho ya kuwasilisha majina ya wagombea.
‘Sina nia’
Ceferin, 58, ambaye ametajwa kama mmoja ya wagombea wa nafasi ya Rais wa FIFA, anasema yeye bado amejikita kwenye UEFA.
“Sina nia ya kugombea kwa sababu mbili. Sababu ya kwanza naipenda UEFA na napenda kufanya kazi hapa, na nadhani wakati fulani … ni wakati wa kufurahia maisha.
“Na la pili ni kuwa, sifa yangu itakuwa juu, juu zaidi iwapo sitogombea.”
Alipoulizwa kama Infantino amekuwa karibu sana na Rais Donald Trump, zaidi kabla ya mashindano ya Kombe la Dunia, Ceferin alisema: “Kwa kweli, utakuwa limbukeni kudhani kuwa mwanasiasa kama huyo, au mwanasiasa yoyote, ni rafiki wa dhati. Kipindi unakuwa na tatizo, unakuwa si rafiki tena wa mwanasiasa.”














