Serikali ya Afrika Kusini na kundi la kutetea jamii ya Afrikaner siku ya Jumatano walipinga msimamo wa serikali ya Marekani kuwa kuna hali ya dharura ambapo wazungu wa Afrika Kusini wanapitia changamoto.
Msimamo huu umetumika kama kigezo kuongeza idadi ya wakimbizi Marekani, lakini kwa Afrikaner wazungu pekee. Serikali ya Trump ilisema Jumanne itawapokea raia wa Afrika Kusini 10,000 zaidi mwaka huu, kuongeza idadi yake ya kila mwaka, lakini kuzuia watu kutoka nchi zingine kuingia kupitia mpango huo.
Tangazo hilo la Rais wa Marekani Donald Trump lilisema wanaongeza idadi ya wakimbizi watakaowapokea kwa sababu ya “dharura isioepukika ya wakimbizi.”
Idara ya mambo ya nje ya Afrika Kusini ilisema Jumatano kuwa madai ya mateso kwa wazungu wa Afrikaner hayana msingi, ikieleza kuwa baadhi ya wale waliopata fursa ya kwenda Marekani kama wakimbizi wameamua kurudi Afrika Kusini.











