| Swahili
ULIMWENGU
3 dk kusoma
Hamas yakubali kusalimisha silaha nzito katika 'uamuzi mgumu' kama sehemu ya makubaliano
Kundi la Wapalestina linaendelea na awamu ya pili ya mpango wa kusitisha mapigano Gaza unaoongozwa na Donald Trump.
Hamas yakubali kusalimisha silaha nzito katika 'uamuzi mgumu' kama sehemu ya makubaliano
Mwonekano wa Gaza baada ya shambulio la Israel katika mtaa wa Rimal, Wapalestina wengi waliuawa na kujeruhiwa, mnamo tarehe 29 Julai.

Kundi la Hamas la Palestina limekubaliana na maandishi kwa ajili ya awamu ya pili ya usitishaji mapigano Gaza, yakiegemea kwenye ahadi za pande zote mbili zinazopaswa kutekelezwa kwa wakati mmoja; haya yalisemwa na afisa mwandamizi wa Hamas, Ghazi Hamad, alipozungumza na shirika la habari la Anadolu siku ya Ijumaa.

Hata hivyo, utekelezaji wa ahadi hiyo ya kundi hilo unategemea Israel kutekeleza kikamilifu awamu ya kwanza, kipindi ambacho jeshi la Israel limeendelea kushambulia na kuua raia katika eneo hilo la Palestina lililokumbwa na uharibifu mkubwa.

Hamad, ambaye ni mjumbe wa ofisi ya kisiasa ya Hamas na ujumbe wake wa mazungumzo, alisema kundi hilo limeidhinisha "makubaliano ya wazi na ya maandishi" yanayohusu kuondoka kwa Israel kutoka Ukanda wa Gaza, ujenzi upya, kupelekwa kwa vikosi vya kimataifa, kuanza kazi kwa Kamati ya Kitaifa ya Usimamizi wa Gaza, na mipango inayohusu silaha.

Alisema utekelezaji wa awamu ya pili unategemea Israel kwanza kutimiza wajibu wake wote wa awamu ya kwanza, akiongeza kuwa makubaliano hayo yanapaswa kuchukuliwa kama kifurushi kimoja kilichounganishwa.

"Kama Israel haitatekeleza (wajibu wake chini ya makubaliano hayo), nasi hatutatekeleza yetu," alisema Hamad.

Kuhusu suala la silaha, Hamad alisema makubaliano hayo yanaelekeza kuwa silaha nzito ziwekwe chini ya usimamizi wa Kamati ya Kitaifa ya Usimamizi wa Gaza wakati vipengele vingine vikitekelezwa.

Vipengele hivyo, alisema, vinajumuisha kuondoka taratibu kwa Israel kutoka Gaza hadi kuondoka kabisa, Kamati ya Kitaifa kuanza majukumu yake, kupelekwa kwa vikosi vya kimataifa, na kuvunjwa kwa makundi ya watu wenye silaha yanayofanya kazi kwa niaba ya Israel.

Hamad alisema makubaliano hayo pia yanajumuisha kuundwa kwa kamati ya kimataifa ya usimamizi ili kufuatilia utekelezaji wake kwa kuendelea.

Alisema Hamas itashiriki katika duru mpya ya mazungumzo katika siku zijazo ili kukamilisha taratibu za utekelezaji na ratiba za muda.

Ujumbe wa mazungumzo wa kundi hilo unatarajiwa kukutana na wapatanishi, wawakilishi wa Marekani, na Nikolay Mladenov, ambaye Hamad alimtaja kama mwakilishi mkuu wa Bodi ya Amani.

Hamad alibainisha kuwa Israel haijatangaza rasmi kuidhinisha makubaliano hayo.

Aliyataja makubaliano hayo kuwa "yenye maumivu na magumu" kwa Hamas, akisema kundi hilo lilikuwa na matumaini ya makubaliano bora zaidi lakini likayakubali kutokana na hali halisi Gaza, "mauaji ya kimbari" yanayoendelea, na janga la kibinadamu.

Hamas ilikubali makubaliano hayo ili kuepusha uharibifu zaidi Gaza na kuizuia Israel kutekeleza mpango wa kuwahamisha kwa nguvu Wapalestina kutoka eneo hilo. Hamad aliongeza kuwa makubaliano hayo yalifuatia "mashauriano ya kitaifa ya Wapalestina na mikutano na makundi ya Kipalestina" ili kuhakikisha kuwepo kwa msimamo wa pamoja na wenye maridhiano miongoni mwa Wapalestina.

CHANZO:AA