Trump haridhishwi na Iran inavyoendesha Mlango-Bahari wa Hormuz

Rais Donald Trump amesema kuwa hayo “siyo makubaliano” yaliyofikiwa kati ya Marekani na Iran, akiionya Iran dhidi ya kutoza ushuru kwa meli zinazopita.

By
Mvutano umeongezeka zaidi baada ya Iran kupendekeza kutoza ushuru kwa meli - ingawa hapo awali Trump ametoa maoni kama hayo. / / AA

Rais wa Marekani, Donald Trump, ameilaumu Iran kwa kila anachodai kufanya “kazi mbaya sana” kuhusu suala la kuruhusu mafuta kupita katika Mlango Bahari wa Hormuz na kwa kukiuka masharti ya makubaliano yao ya kusitisha mapigano kwa muda wa wiki mbili.

Katika msururu wa machapisho kwenye mitandao ya kijamii Alhamisi, yaliyoongeza hofu mpya kuhusu kusitishwa kwa mapigano ambako tayari ni dhaifu, Trump pia aliitishia Iran dhidi ya kutoza ushuru kwa meli zinazopita kwenye njia hiyo muhimu ya maji.

“Iran inafanya kazi mbaya sana, wengine wanaweza kusema ya aibu, katika kuruhusu Mafuta kupita katika Mlango wa Hormuz,” Trump alisema kwenye jukwaa lake la Truth Social.

“Hayo si makubaliano tuliyokubaliana!”

Iran na Marekani zilisema kuwa mlango huo wenye urefu wa kilomita 167 kati ya Ghuba na Bahari ya Hindi ungefunguliwa tena baada ya kusitishwa kwa mapigano kwa wiki mbili kutangazwa Jumanne na Pakistan.

Hata hivyo, meli 10 tu ndizo zimepita tangu kusitishwa kwa vita Mashariki ya Kati kuanze kutekelezwa, kulingana na takwimu za ufuatiliaji wa baharini.

Mvutano umeongezeka zaidi baada ya Iran kupendekeza kutoza ushuru kwa meli — ingawa Trump mwenyewe aliwahi kutoa mapendekezo kama hayo na hata kuzungumzia uwezekano wa ushuru wa pamoja na Tehran.

“Kuna ripoti kwamba Iran inatoza ada kwa meli za mafuta zinazopita katika Mlango wa Hormuz — Ni bora isiwe hivyo, na kama ni kweli, basi waache mara moja!” Trump alisema katika ujumbe mwingine kupitia mtandao wake wa Truth Social.

Katika chapisho lingine ambapo alionyesha hasira dhidi ya tahariri ya vyombo vya habari iliyokosoa makubaliano ya kusitisha mapigano, Trump aliongeza kuwa “kwa haraka sana, utaona mafuta yakianza kusafirishwa, iwe kwa msaada wa Iran au bila msaada.”

Mauaji ya Lebanon

Mtazamo wa kiongozi huyo wa Marekani ulionekana kuwa mkali zaidi ikilinganishwa na maoni yake ya awali kwa NBC News, ambapo alisema alikuwa “na matumaini makubwa” kuhusu makubaliano ya amani na Iran baada ya kusitishwa kwa mapigano, na kwamba Israel ilikuwa “ikipunguza” mashambulizi yake dhidi ya Lebanon.

Trump aliiambia televisheni hiyo ya Marekani katika mahojiano ya simu kwamba viongozi wa Iran walikuwa “wenye mantiki zaidi” faraghani, lakini akaongeza kuwa “kama hawatafanya makubaliano, hali itakuwa chungu sana.”

Makamu wa Rais JD Vance anatarajiwa kufanya mazungumzo na Iran huko Pakistan Jumamosi. Mjumbe maalum Steve Witkoff na mkwe wa Trump, Jared Kushner, pia wanasafiri kuelekea Islamabad.

“Rais ana matumaini kuwa makubaliano yanaweza kufikiwa ambayo yanaweza kuleta amani ya kudumu Mashariki ya Kati,” Naibu Msemaji Mkuu wa Ikulu, Anna Kelly, aliambia AFP katika taarifa Alhamisi.

Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, wakati huo huo alikubali katika mazungumzo na simu na Trump Jumatano “kupunguza makali” ya mashambulizi dhidi ya Lebanon baada ya Israel kutekeleza mashambulizi makubwa, Trump alisema.

Israel na Lebanon zitafanya mazungumzo mjini Washington wiki ijayo, afisa wa Wizara ya Mambo ya Nje alisema Alhamisi.

Mashambulizi makubwa ya anga ya Israel dhidi ya Lebanon Jumatano yaliua zaidi ya watu 300, wengi wao wakiwa raia, na kuyumbisha usitishaji wa mapigano ambao tayari haukuwa thabiti kati ya Washington na Tehran chini ya saa 48 tangu uanze kutekelezwa.