Ndege mpya ya Air Force One aliyotumia Rais Donald Trump kusafiria Uturuki haina baadhi ya mifumo ya kujihami iliyokuwepo kwenye ndege ya awali ya rais, ikiwemo uwezo wa hali ya juu wa kujikinga dhidi ya makombora, kwa mujibu wa ripoti ya gazeti la The New York Times iliyowanukuu maafisa wa Marekani.
Wataalamu wanaonya kuwa Boeing 747-8 aliyozawadiwa na Qatar inaweza kuongeza kiwango cha hatari katika safari za kimataifa, huku ripoti zikidai kuwa Walinzi Rasmi wa Viongozi Marekani walimshauri Trump kurudi Marekani kwa kutumia Air Force One ya zamani.
Ikulu ya White House ilitetea usalama wa ndege hiyo, lakini haikutoa maelezo kuhusu uwezo mahsusi. Msemaji wa Ikulu, Steven Cheung, alisema: "Air Force One mpya ni ndege ya kisasa yenye viwango vya juu vya usalama ambayo imewekewa mifumo madhubuti ya kulinda usalama wa rais na wafanyakazi wake."
Jeshi la Anga la Marekani limekiri kuwa ndege hiyo haina vifaa vyote vinavyohitajika kwenye Air Force One . Limeieleza kuwa ni ndege ya muda itakayotumika hadi ndege mbili mpya za rais zinazotengenezwa na Boeing zitakapokamilika.
Katika taarifa ya Juni 19, Jeshi la Anga lilisema: "Wamechukua tahadhari zote za kiusalama, ulinzi na mawasiliano ya misheni."
Hata hivyo, maafisa wanaofahamu mchakato wa maboresho ya ndege hiyo walisema haijapewa mifumo sawa ya kujihami dhidi ya mashambulizi kama ilivyokuwa kwa ndege ya awali, ingawa Jeshi la Anga halijabainisha ni mifumo gani hasa iliyoachwa.
Maafisa wawili wa zamani wa Jeshi la Anga waliokuwa sehemu ya mpango wa kubadilisha ndege ya rais walisema walishangazwa na uamuzi wa Trump kuitumia ndege hiyo katika safari ya nje ya nchi, wakieleza kuwa mazingira ya usalama katika safari hizo huwa na hatari kubwa zaidi.
Waliongeza kuwa kasi ya maandalizi huenda haikuruhusu muda wa kutosha wa kufunga mifumo yote ya usalama ambayo kwa kawaida hupatikana kwenye Air Force One iliyokamilika.















