Iran yaiambia Lebanon, kuwa balozi wake ataendelea kuwepo nchini humo licha ya kufukuzwa

Wiki iliopita, wizara ya Mambo ya Nje ya Lebanon inasema kuwa imemtaka balozi mteule wa Iran Mohammad Reza Shibani na kumtaka aondoke nchini kufikia Machi 29.

By
Mamlaka za Lebanon zimemshtumu Mohammad Reza Shibani kukiuka kanuni za kidiplomasia kwa matamshi yake kuhusu siasa za ndani. [Picha ya maktaba] / AFP

Iran imesema siku ya Jumatatu kuwa balozi wake nchini Lebanon ataendelea kuwepo katika wadhifa wake mjini Beirut, akipingana na Wizara ya Mambo ya Nje ya Lebanon, ambayo imemtimua nchini humo na kumtaka kuondoka.

Huku vita vikirindima nchini Lebanon kati ya Hezbollah na Israel, hadhi ya balozi wa Iran imesababisha mvutano kati ya kundi la Shia linaloungwa mkono na Iran na serikali ya Lebanon, ambayo imeshtumu Hezbollah kwa kuingilia vita katika kanda kuunga mkono Iran.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Lebanon wiki iliopita ilisema imeamua kufuta vyeti vya balozi mteule wa Iran, Mohammad Reza Shibani, na kumtaka aondoke nchini humo kufikia Machi 29.

Wizara hiyo inasema wakati huo Shibani alikuwa amekiuka utaratibu wa kidiplomasia kwa kutoa matamshi kuhusu siasa za ndani za Lebanon.

Spika wa Bunge la Lebanon Nabih Berri, mwanasiasa mwenye ushawishi mkubwa kwa Waislamu wa Shia na mshirika wa Hezbollah, amepinga uamuzi wa Wizara ya Mambo ya Nje na kumtaka Shibani kubaki katika wadhifa wake, vyanzo vinavyomfahamu Berri vilisema.

‘Balozi wa Iran ataendelea kuwepo kwenye nafasi yake’

Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje wa Iran Esmail Baghaei, akizungumza na waandishi wa habari, alisema kuwa Shibani ataendelea kubaki mjini Beirut.

"Kwa kuzingatia majadiliano yaliyofanywa na pande zote nchini Lebanon na kufikia makubaliano, balozi wa Iran ataendelea kazi zake za ubalozi mjini Beirut na bado yuko huko," Baghaei alisema.

Wizara ya Mambo ya Nje ya Lebanon haijatoa taarifa yoyote kuhusu suala hilo licha ya muda wa mwisho kupita, na haikujibu ombi la kutaka izungumzie hilo.

Lebanon iliingia katika vita vya Mashariki ya Kati Machi 2, wakati Israel na Marekani ilipoanza vita dhidi ya Iran, kumuua Kiongozi Mkuu Ali Khamenei, kusababisha kundi la Shia la Hezbollah washirika wa Iran kurusha makombora dhidi ya maeneo ya Israel.

Tangu wakati huo, Israel imezidisha mashambulizi yake Lebanon na kuendeleza kusini mwa nchi, kuwaua watu zaidi ya 1,200 nchini Lebanon na watu zaidi ya milioni 1 kuondoka katika makazi yao.

Waziri Mkuu wa Lebanon Nawaf Salam, ambaye serikali yake imekuwa ikitaka kuwapokonya silaha Hezbollah kwa njia ya amani, anasema uamuzi wa kushambulia Israel ni kinyume na matakwa ya raia wengi wa Lebanon na kupiga marufuku kikosi chake cha jeshi.