Watu wasiopungua 14 wameuawa, ikiwemo watoto sita, katika tukio la wizi wa ng’ombe kaskazini mwa Sudan Kusini, afisa mmoja wa eneo hilo ameiambia AFP siku ya Jumatano.
Shambulio hilo lilitokea Jumanne usiku eneo la Padang Payam Jimbo la Unity.
"Kumekuwa na mashambulizi ya vijana wenye silaha kutoka eneo la Ruweng, na waliwaua watu wasiopungua 14 asubuhi hii, ikiwemo watoto sita, wanaume sita, mwanamke mmoja na msichana mmoja," Waziri wa Habari wa Jimbo la Unity Nyakenya Johannes Keah alisema, akiongeza kuwa idadi hiyo huenda ikaongezeka.
Ng’ombe karibu 200 waliibiwa wakati wa shambulizi hilo na kupelekwa Ruweng, aliongeza.
Taarifa zinaonya mashambulizi zaidi jimbo la Jonglei
Waziri wa habari katika eneo la Ruweng, Salva Nyok, alikanusha madai hayo katika mawasiliano kwa njia ya simu na AFP.
Taarifa ya usalama kutoka Jumatatu, ambayo ilishuhudiwa na AFP, ilionya kuwa vijana walikuwa wanahamasishwa kuiba ng’ombe katika jimbo la Jonglei, ambako kumekuwa na mapigano makali kati ya vikosi vya serikali na upinzani.
"Pamoja na kuwa lengo lilotajwa ni wizi wa ng’ombe, kuna hatari ya vurugu kuendelea zaidi ya wizi huo na kujumuisha wanasiasa na masuala ya kijamii," taarifa hiyo ilisema.


















