Russia, Ukraine zakabidhiana miili ya wanajeshi waliouwawa
Urusi imesema kuwa miili ya askari 1,000 imepelekwa Ukraine, huku miili mingine 38 ikirudishwa Urusi.
Urusi na Ukraine zimekamilisha makabidhiano ya wanajeshi waliouwawa vitani, ikiwa ni sehemu ya makubaliano kati ya nchi hizo, yaliyofikiwa mwaka huu jijini Istanbul.
Katika taarifa kupitia jukwaa la Telegram, mpambe wa rais wa Urusi, Vladimir Medinsky alisema kuwa jumla ya miili 1,000 ya wanajeshi hao ilipelekwa Ukraine, huku miili mingine 38, ikikabidhiwa Urusi.
"Kupitia makubaliano yetu ya Istanbul, miili ya askari 1,000 imepelekwa Ukraine. Miili mingine ya wanajeshi 38, ikipelekwa nchini Urusi," alisema.
Kwa upande mwingine, kupitia taarifa yake, Makao Makuu ya Uratibu ya makabidhiano ya Wafungwa wa Kivita ya nchini Ukraine, ilithibitisha makabidhiano hayo, ikisema kuwa imepokea miili ya wanajeshi 1,000.
Disemba 30, Naibu Waziri wa Mambo ya Nje Mikhail Galuzin, alisema kuwa takribani wanajeshi 2,300 na raia 170, walirudishwa Ukraine chini ya mkataba wa Istanbul.