Mjue Lordina Mahama, mke wa Rais wa Ghana
Lordina Mahama, mke wa rais wa Ghana /Picha:@MrsMahama
Mjue Lordina Mahama, mke wa Rais wa Ghana
Yeye ndiye mwanzilishi na rais wa Taasisi ya Lordina (Lordina Foundation), shirika la hisani linalotoa ufadhili wa masomo, kusaidia vituo vya watoto yatima na kuwezesha vifaa katika wodi za wazazi na watoto.

Lordina Mahama ndiye Mke wa Rais wa Ghana kwa sasa, akiwa amerejea katika wadhifa huo Januari 7, 2025 baada ya kuapishwa kwa mume wake, Rais John Dramani Mahama.

Hii ni mara yake ya pili kushika nafasi ya Mke wa Rais wa Ghana.

Aliwahi kushika nafasi hiyo awali kuanzia mwaka 2012 hadi 2017, wakati mume wake alipokuwa rais kabla ya kushindwa uchaguzi.

Hali hii inamfanya kuwa mmoja wa wanawake wachache katika historia ya Ghana kuwa mke wa rais kwa awamu mbili tofauti.

Amezaliwa Machi 1963 katika Mkoa wa Bono East nchini Ghana, Lordina Mahama alipata elimu yake ya awali mjini Tamale kabla ya kusoma katika Shule ya Sekondari ya Ghana, ambapo ndipo alipokutana na mume wake.

Yeye ni mtaalamu katika sekta ya huduma akiwa na shahada katika Usimamizi huduma na Utawala na Uongozi kutoka Taasisi ya Ghana Institute of Management and Public Administration (GIMPA).

Pia amesoma katika Chuo Kikuu cha De Montfort nchini Uingereza.

Katika kipindi chote cha safari ya kisiasa ya mume wake, Lordina Mahama amekuwa na jukumu la kutoa ushirikiano hadharani huku akiipigia debe mipango ya maendeleo ya kijamii.

Akiwa Mke wa Rais, amejikita katika kuboresha huduma za afya kwa mama na mtoto, kukuza uwezeshaji wa wanawake, kusaidia elimu ya ufundi na ujuzi, kuhamasisha uelewa kuhusu saratani ya matiti na mlango wa kizazi pamoja na UKIMWI, na kusaidia vituo vya watoto yatima na jamii zilizo katika mazingira magumu.

Yeye ndiye mwanzilishi na rais wa Taasisi ya Lordina (Lordina Foundation), shirika la hisani linalotoa ufadhili wa masomo, kusaidia vituo vya watoto yatima, kuwezesha vifaa katika wodi za wazazi na watoto, kuendesha programu za huduma za afya kwa jamii, kutoa vifaa vya hospitali, na kukuza mafunzo ya ujuzi na uwezeshaji wa kiuchumi kwa wanawake na wasichana.

Tangu mume wake kurudi madarakani mwaka 2025, Lordina Mahama ameendelea kutetea uboreshaji wa huduma za afya na ustawi wa jamii.

Katika mwaka huu wa 2026, amezindua vituo vipya vya afya ya mama na mtoto, kuhamasisha mipango ya uzazi salama, na kupokea utambuzi wa kimataifa kutoka Taasisi ya Merck kutokana na kazi yake ya muda mrefu ya kibinadamu kupitia Taasisi ya Lordina.

Lordina na Mahama walifunga ndoa mwaka 1992 na wana watoto watano. Katika kipindi chote cha safari ya kisiasa ya mume wake, amekuwa mstari wa mbele katika kudumisha nafasi ya huduma kwa umma, akiunga mkono kampeni za mume wake pamoja na mipango yake ya kitaifa na kimataifa.

CHANZO:TRT Swahili