Wake wa Marais wa Afrika: Mary Ayen Mayardit wa Sudan Kusini
Mary Mayardit ni mke wa Rais wa Sudan Kusini , Salva Kiir/picha:@ssemtv / Public domain
Wake wa Marais wa Afrika: Mary Ayen Mayardit wa Sudan Kusini
Kabla ya uhuru wa Sudan Kusini, Mary Ayen Mayardit alikuwa mpigania ukombozi aliyejitolea wakati wa mapambano ya miaka 21 dhidi ya Sudan.

Mary Ayen Mayardit, anayejulikana maarufu kama "Mama Mary," nchini mwake, ni Mke wa Rais wa sasa wa Jamhuri ya Sudan Kusini, Salva Kiir.

Amekuwa katika nafasi hiyo tangu uhuru wa nchi hiyo Julai 2011.

Huu ni wakati ambao mume wake Rais Salva Kiir Mayardit alipochukua urais wa taifa hilo changa zaidi barani Afrika.

Kabla ya uhuru wa Sudan Kusini, alikuwa mpigania ukombozi aliyejitolea wakati wa mapambano ya miaka 21 dhidi ya Sudan.

Kwa heshima ya juhudi zake za kijeshi, Rais Salva Kiir alimpandisha cheo na kuwa Meja Jenerali katika jeshi la Sudan Kusini mwaka 2020.

Mary Mayardit mara nyingi maisha yake sio ya hadharani, lakini bado ana ushawishi mkubwa katika utetezi wa kitaifa, ujenzi wa amani, na mifumo ya umoja ndani ya Sudan Kusini.

Nchi yake ilitumbukia katika mzozo wa ndani mwaka 2013 ambao ulisababisha vifo vya takriban 400,000 na mamilioni ya watu kuyahama makazi yao huku wengine wakitafuta hifadhi nje ya nchi.

Kwa hivyo kazi yake kwa muda imeegemea zaidi kusaidia watu wa nchi yake ambao waliathiriwa.

Alianzisha shirika linaloitwa "Concern South Sudan," shirika lisilo la kiserikali linalojitolea kuwawezesha wanawake na vijana, kupeleka chakula, elimu, na misaada ya matibabu katika jamii zilizoathiriwa na zisizojiweza.

Mama Mary amekuwa akilitumia jukwaa lake mara kwa mara kupinga ndoa za utotoni, kukuza elimu ya wasichana, na kusukuma usawa wa wanawake na wanaume serikalini.

Amesifiwa na waangalizi wa kisiasa kwa kusaidia kupunguza migawanyiko wakati wa mazungumzo ya amani yenye changamoto na anasalia kuhusika kwa kina katika kuunga mkono mipango ya kilimo na maendeleo ya jamii.

Akiwa katika jamii ambayo bado haijapona kutokana na mgawanyiko wa kikabila mara nyingi anachukua jukumu la kuwaunganisha hasa wanawake.

Kupitia utetezi wake na ushiriki wa hali ya juu, ametetea upatanisho wa kihistoria na kuhimiza pande zinazopingana kuweka silaha chini ili kuleta utulivu nchini.

Na kibara Mary Mayardit anawakilisha Sudan Kusini kama mwanachama wa Shirika la Wake wa Marais wa Afrika kwa Maendeleo (OAFLAD), akishirikiana na wenzake barani kushughulikia afya, kupunguza umaskini, na kutetea haki za wanawake.

CHANZO:TRT Swahili