Marekebisho ya katiba yanayopendekezwa katika Seneti ya Kenya yanazua mjadala baada ya wabunge kuwasilisha Mswada ambao utawazuia waliokuwa magavana wa kaunti kuwania viti vya Mbunge (MP) au Mwakilishi wa Kaunti (MCA) kwa kipindi cha miaka mitano baada ya kuondoka afisini.
Mswada wa Katiba ya Kenya (Marekebisho) wa 2026 unalenga kuwasilisha kile ambacho wabunge wanakiita “kipindi cha mapumziko” kinacholenga kurekebisha mabadiliko ya kisiasa kutoka kwa uongozi wa kaunti hadi afisi zingine za uchaguzi.
Iwapo itapitishwa, sheria hiyo itawazuia magavana wa zamani kugombea viti vya Mbunge au MCA mara moja, kuweka muda wa kusubiri wa miaka mitano baada ya kuondoka afisini na kuwaruhusu kugombea nyadhifa za juu pekee kama vile Rais au Naibu Rais katika kipindi hicho.
Pendekezo hilo tayari limewasilishwa katika Seneti na kupelekwa kwa Kamati ya Kudumu ya Haki, Masuala ya Kisheria na Haki za Kibinadamu kwa ajili ya kuzingatiwa, na kuashiria kuwa bado katika hatua ya awali ya kutunga sheria.
Mikutano ya ushiriki wa umma pia imeratibiwa kuendeshwa hadi tarehe 8 Mei, kumaanisha kuwa Wakenya watakuwa na nafasi ya kuwasilisha maoni yao kabla ya Mswada huo kuendelea zaidi.
Kupunguza urejeleaji wa kisiasa
Wafuasi wa Mswada huo wanahoji kuwa unasukumwa na masuala matatu makuu, hasa uwajibikaji na kukamilika kwa ukaguzi.
Wabunge wanasema magavana hushughulikia bajeti kubwa za kaunti, na michakato ya ukaguzi wa Mkaguzi Mkuu wa Hesabu na Seneti mara nyingi huongeza zaidi ya muda wao.
Kipindi cha "mapumziko" kinanuiwa kuhakikisha michakato hii ya uangalizi inakamilika bila kuingiliwa na magavana wa zamani ambao bado wanaweza kuwa na ushawishi wa kisiasa.
Kuna wasiwasi pia kwamba gavana wa zamani kuwa mbunge au MCA, hasa katika kaunti hiyo, kunaweza kudhoofisha usimamizi, kwa kuwa afisi hizo zinahusika moja kwa moja katika kukagua matumizi na utawala wa kaunti.
Ng’ang’anizi madarakani
Mswada huo pia unalenga kukatisha tamaa kile ambacho baadhi ya wabunge wanakiita "ushukaji hadhi" katika siasa, ambapo magavana walio na ukomo wa muda huhamia mara moja viti vingine vya kuchaguliwa badala ya kuruhusu uongozi mpya kuibuka.
Hata hivyo wapinzani, ikiwa ni pamoja na baadhi ya wataalam wa sheria, wanasema pendekezo hilo linaweza kukiuka haki za kikatiba chini ya Ibara ya 38, ambayo inawahakikishia raia haki ya kugombea nafasi ya kuchaguliwa, kulenga isivyo haki kundi maalum la viongozi au kufutwa na mahakama iwapo itapingwa.
Pia wanahoji kuwa wapiga kura, sio sheria, wanapaswa kuamua kama gavana wa zamani anafaa kwa ofisi nyingine.
Sheria nchini Kenya inawaruhusu magavana kugombea kwa mihula 2 pekee lakini baadhi ya magavana wa zamani huko nyuma wamewania viti vya chini kusalia mamlakani.






















