Uturuki na Afrika: Safari ya ushirikiano wa muda mrefu na matumaini mapya
Afrika inavyoendelea kujenga mustakabali wake, mtindo wa ushirikiano wa Uturuki unaojengwa juu ya heshima, uwepo wa karibu, na kujitolea kwa muda mrefu unaonekana kuwa mchango chanya na wa kudumu katika safari ya bara hilo kuelekea maendeleano.
Mohamed Ahmed Alasow alikuwa na umri wa miaka kumi wakati aliyekuwa Waziri Mkuu wa wakati huo, Recep Tayyip Erdogan, alipotembelea mji wa Mogadishu mwaka 2011.
Wakati huo, Somalia ilikuwa ikijinasua kutoka katika moja ya vipindi vigumu zaidi katika historia yake ya kisasa; njaa kali, migogoro, na kutekelezwa kimataifa vilikuwa vikifafanua maisha ya kila siku kwa miaka kadhaa.
Kwa Wasomali wengi waliokuwa na umri wa Mohamed, ziara hiyo haikuwa tu tukio la kidiplomasia; ilikuwa ni wakati wa matumaini. Kumwona kiongozi wa kigeni akitembea waziwazi mitaa ya Mogadishu, akizungumza moja kwa moja na wananchi wa kawaida, na kuonyesha mshikamano badala ya kujitenga, lilikuwa jambo la kihistoria.
Ilikuwa ni hatua ya mabadiliko si tu katika uhusiano kati ya Somalia na Uturuki, bali pia katika namna Wasomali walivyoanza kufikiria nafasi ya nchi yao katika ulimwengu mpana.
Hatua ya mabadiliko
Tukio hilo lilibaki moyoni mwa Mohamed. Miaka kadhaa baadaye alikuja Uturuki kusomea Sayansi ya Siasa na Mahusiano ya Kimataifa katika Chuo Kikuu cha Medipol University kilichopo Istanbul.
Leo hii, akiwa Mwenyekiti wa Chama cha Wanafunzi wa Kisomali nchini Uturuki (UMASET), Mohamed mara nyingi hutafakari jinsi uzoefu huo wa awali ulivyoathiri safari yake ya kitaaluma na maisha yake binafsi. Kusoma nchini Uturuki kulimnufaisha kwa kiasi kikubwa.
Kulimfungulia macho kuhusu ulimwengu, kumuweka karibu na tamaduni tofauti, na kumpa mtazamo mpana wa kimataifa. Kusoma pamoja na wanafunzi kutoka mataifa mbalimbali katika mazingira ya kitaaluma yaliyounganishwa kwa karibu na diplomasia halisi kulimsaidia kuelewa vyema uongozi, ushirikiano, na mahusiano ya kimataifa.
Safari yake binafsi inaakisi hadithi pana ya uhusiano kati ya Uturuki na Afrika uliokua katika muongo uliopita.
Ushirikiano wa Uturuki na Somalia ulianza kwa msaada wa kibinadamu wakati wa mgogoro wa mwaka 2011, lakini haukuishia hapo. Baadaye uliendelea na kuwa ushirikiano wa kina na wa kimfumo unaotegemea dhamira ya muda mrefu.
Badala ya kuishia kwenye misaada ya dharura pekee, Uturuki ilijizatiti moja kwa moja nchini Somalia kama mshirika katika kujenga upya uwezo wa taasisi za dola.
Kufunguliwa upya na kuimarishwa kwa taasisi za umma mjini Mogadishu, uwekezaji katika miundombinu ya afya na elimu, pamoja na msaada katika masuala ya usalama na utawala, ni matokeo yanayoonekana ya mkabala huu.
Kwa kufanya kazi moja kwa moja na taasisi za Kisomali na kuwaweka wadau wa ndani katikati ya mchakato, Uturuki ilisaidia kukuza mtindo wa ushirikiano unaozingatia umiliki wa ndani, heshima, na uendelevu.
Mkakati huu hauishii Somalia pekee; unaakisi falsafa pana inayobainisha ushiriki wa Uturuki kote barani Afrika. Kinachotofautisha mchango wa Uturuki barani humo ni mtazamo wake unaomweka mwananchi mbele na kufanya kazi moja kwa moja mashinani.
Katika sekta ya afya, hili linaonekana kupitia hospitali zinazotoa huduma bora na zinazofikika kwa wananchi wa kawaida. Katika miundombinu, linaonekana kupitia ujenzi wa barabara, viwanja vya ndege, na majengo ya umma yanayoboreshwa maisha ya kila siku.
Katika elimu, linaonekana kupitia uwekezaji wa muda mrefu katika rasilimali watu, ikiwemo ufadhili wa masomo, ujenzi wa shule, na ushirikiano wa kitaaluma.
Badala ya kufanya kazi kwa mbali, Uturuki hufanya kazi bega kwa bega na wenyeji, husikiliza mahitaji yao, na kutoa matokeo yanayoonekana na kuguswa na wananchi.
Daraja la kudumu
Elimu imekuwa moja ya madaraja ya kudumu kati ya Uturuki na Afrika. Maelfu ya wanafunzi wa Kiafrika wamesoma katika vyuo vikuu vya Uturuki na kurejea makwao wakiwa na ujuzi, mitandao ya kimataifa, na uelewa mpana wa ushiriki wa kimataifa.
Wanafunzi hawa si wanufaika wa elimu pekee; ni mabalozi wa baadaye, wataalamu, na viongozi wanaobeba uzoefu halisi wa ushirikiano uliojengwa juu ya heshima ya pande zote.
Huu upande wa kibinadamu unabaki kuwa nguzo muhimu ya sera ya Uturuki kwa Afrika, na sababu kuu inayofanya uwepo wake barani humo kuonekana kuwa wa kuaminika na wa dhati.
Mbali na maendeleo na elimu, Uturuki pia imejitokeza kama mshiriki chanya katika juhudi za kujenga amani na diplomasia barani Afrika.
Hili lilidhihirika mwaka jana wakati Uturuki ilipoandaa mazungumzo kati ya Somalia na Ethiopia, ikitoa jukwaa la mazungumzo lililo huru na linaloaminika katika wakati nyeti wa uhusiano wa mataifa hayo mawili.
Katika Pembe ya Afrika, ushirikiano wake umejikita kwenye mazungumzo, upatanishi, na uimarishaji wa uwezo wa ndani kama michakato inayofaidisha pande zote.
Badala ya kuzingatia tu utatuzi wa migogoro ya muda mfupi, Uturuki inalenga kuimarisha uwezo wa wadau wa ndani kushughulikia changamoto zao wenyewe.
Kwa kuweka wazi njia za mawasiliano, kuunga mkono uimara wa taasisi, na kuepuka masuala yanayoongeza mgawanyiko, Uturuki inachangia katika kuleta utulivu kwa njia ya makini.
Kanuni kama hizi pia zinaongoza ushiriki wa Uturuki katika maeneo mengine ya bara. Kaskazini mwa Afrika, ushiriki wake nchini Libya umechanganya juhudi za kidiplomasia na msaada kwa mazungumzo ya kisiasa.
Nchini Sudan, Uturuki imeendelea kuunga amani na kutoa msaada wa kibinadamu.
Katika Ukanda wa Sahel na Afrika Magharibi, ushirikiano wa maendeleo, mafunzo ya usalama, na msaada wa taasisi unalenga kuimarisha utulivu huku ukishughulikia mahitaji ya muda mrefu ya kijamii na kiuchumi.
Juhudi hizi zinaakisi uelewa mpana kwamba amani, maendeleo, na utawala bora vimefungamana kwa karibu.
Diplomasia inayowezesha
Kwa mujibu wa Dk. Tunç Demirtaş, mtafiti wa sera za nje katika Taasisi ya SETA Foundation, nguvu ya Uturuki barani Afrika ipo katika diplomasia yake inayowezesha.
Kwa kujiweka kama mshiriki wa kuaminika na sio kama mshindani katika mvutano wa kijiografia wa kimataifa, Uturuki hujenga imani na mahusiano ya muda mrefu. Msisitizo wake katika muunganiko, ushirikiano, na uimarishaji wa uwezo wa ndani husaidia kupunguza mazingira yanayochochea migogoro.
Mfumo huu wa uwiano—unaounganisha mazungumzo na msaada wa kivitendo—umeiwezesha Uturuki kuwa na nafasi ya kuleta utulivu bila kulazimisha suluhisho kutoka nje.
Kuanzia mtoto wa Kisomali wa miaka kumi aliyeshuhudia ziara ya kihistoria mwaka 2011 hadi kizazi kipya cha wanafunzi wa Kiafrika wanaosoma nchini Uturuki leo, nyayo za Uturuki barani Afrika zinaonekana.
Ni misingi iliyojengwa si tu kwa miradi na sera, bali pia kwa mahusiano, uzoefu wa pamoja, na dhamira endelevu.
Kadri Afrika inavyoendelea kuunda mustakabali wake, mtindo wa ushirikiano wa Uturuki unaojengwa juu ya heshima, uwepo, na kujitolea kwa muda mrefu unabaki kuwa mchango chanya na wa kudumu katika safari ya bara hilo kuelekea mbele.
Mwandishi, Hafsa Abdiwahab Sheikh, ni mwandishi wa kujitegemea na mtafiti anayejikita katika siasa za Afrika Mashariki.