Iran imekataa pendekezo la Marekani la kumaliza vita vinavyoendelea, ikisisitiza kuwa suluhisho lolote litategemea kikamilifu masharti na muda wake yenyewe, kulingana na afisa mwandamizi wa kisiasa na usalama.
Afisa wa Iran, akizungumza na Press TV, alisema Iran haitamruhusu Rais wa Marekani, Donald Trump, kuamua mwelekeo wa matukio, akisisitiza kwamba “operesheni za kujihami” zitaendelea hadi masharti yake yatakapotekelezwa.
“Iran itamaliza vita pale itakapoamua kufanya hivyo na pale masharti yake yatakapotekelezwa,” alisema afisa huyo, akiongeza kuwa Tehran iko tayari kuendelea kukabiliana na kutoa “mapigo mazito” hadi malengo yake yatakapofikiwa.
Iran imeainisha masharti matano muhimu kwa ajili ya kukubali kusitisha mapigano. Haya yanajumuisha kusitishwa kabisa kwa kile inachokiita uchokozi na mauaji ya kulenga watu maalum, kuwekwa kwa dhamana za kuzuia vita kuanza tena, pamoja na malipo ya uaribifu na fidia.
Iran pia inadai kukomeshwa kabisa kwa uhasama katika pande zote zinazohusisha makundi washirika katika eneo hilo, pamoja na kutambuliwa kwa mamlaka yake juu ya Mlango wa Hormuz, jambo ambalo inasema ni muhimu kuhakikisha utekelezaji wa makubaliano yoyote.
Afisa huyo alisema masharti haya yanajengwa juu ya misimamo iliyowasilishwa hapo awali katika duru za mazungumzo huko Geneva, zilizofanyika muda mfupi kabla ya ongezeko la hivi karibuni la mvutano lililoanza tarehe 28 Februari.
Iran imewaambia wapatanishi kwamba hakutakuwa na mazungumzo yoyote isipokuwa masharti yake yote yakubaliwe, ikisisitiza kuwa kusitisha mapigano kunategemea utekelezaji kamili wa masharti hayo.
“Mwisho wa vita utatokea pale Iran itakapoamua kuwa vita vinapaswa kumalizika, si pale Trump anavyofikiria vita vitaisha,” alisema afisa huyo.
Iran inaona juhudi za hivi karibuni za Washington, zilizowasilishwa kupitia wapatanishi wa kikanda, kuwa “zimezidi mipaka” na hazilingani na hali halisi katika uwanja wa vita.
Pendekezo hilo limekataliwa na kuonekana kama jaribio la kuongeza mvutano badala ya kuutatua.
Marekani ilituma mpango wa vipengele 15 kwa Iran wa kumaliza vita, kulingana na ripoti ya The New York Times.
Pendekezo hilo liliwasilishwa kupitia Pakistan, ambaye mkuu wa jeshi lake ameibuka kama mpatanishi muhimu kati ya Marekani na Iran.














