Umoja wa Afrika wapongeza mazungumzo kati ya Paul Kagame na Felix Tshisekedi nchini Qatar

Katika kikao hicho, viongozi hao walitoa wito wa kusitishwa kwa machafuko katika eneo la mashariki mwa DRC.

Youssouf pia alionesha utayari wa Umoja wa Afrika katika kuunga mkono mazungumzo ya amani ya Luanda na Nairobi, akisema kuwa kikao cha Doha kinaakisi jitihada mbalimbali za kikanda./@ymahmoudali

Umoja wa Afrika umepongeza hatua ya kiongozi wa Qatar Sheikh Tamin bin Hamad Al Thani, ya kuwakutanisha Rais Paul Kagame wa Rwanda na Felix Tshisekedi wa DRC kwa mazungumzo yaliyofanyika Machi 18, 2025 jijini Doha.

Katika taarifa yake ya Machi 19, 2025, Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika Mahamoud Ali Youssouf, amewapongeza viongozi hao kwa uamuzi wa kufanya majadiliano ili kupata suluhu ya kudumu ya eneo la mashariki mwa DRC.

Mwenyekiti huyo wa Umoja wa Afrika aliwapongeza viongozi hao wawili kwa utayari wao kutafuta suluhu ya machafuko hayo.

“Kikao hicho kinadhihirisha uongozi wa kweli na umuhimu wa amani kwa mataifa yao na eneo zima la Maziwa Makuu,” alisema Youssouf katika taarifa hiyo.

Youssouf pia alionesha utayari wa Umoja wa Afrika katika kuunga mkono mazungumzo ya amani ya Luanda na Nairobi, akisema kuwa kikao cha Doha kinaakisi jitihada mbalimbali za kikanda.

Katika kikao hicho, viongozi hao walitoa wito wa kusitishwa kwa machafuko katika eneo la mashariki mwa DRC.